2014-07-29 10:04:38

Yesu Kristo awe ni kiini cha maisha na utume wa Wakristo!


Mchungaji Giovanni Traettino wa Kanisa la Kipentekoste mjini Caserta, Italia, Siku ya Jumatatu, tarehe 28 Julai 2014, amemshukuru kwa namna ya pekee Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwapatia heshima ya kuwatembelea na kukaa kwa pamoja mbele ya Mwenyezi Mungu. Wakristo hawa wamemhakikishia Baba Mtakatifu Francisko kwamba wanampenda na wanamwombea katika maisha na utume wake na kwamba, kuteuliwa kwake ni zawadi kubwa kutoka kwa Roho Mtakatifu kwa ajili ya Kanisa na Ulimwengu kwa ujumla.

Katika maisha yake, anasema Mchungaji Traettino kwamba, Baba Mtakatifu anaweza kuwaendea watu na kugusa undani wa mioyo yao sanjari na kujenga mahusiano thabiti ya kijamii, kwa kutambua kwamba, wote ni ndugu katika Kristo Yesu, kielelezo cha uhuru na ujasiri katika kutambua mapungufu ya kibinadamu, tofauti zilizopo kati ya Makanisa na matumaini ya kujenga umoja miongoni mwa Wakristo, changamoto endelevu kutoka kwa Yesu mwenyewe.

Ni vigumu sana kujenga umoja pasi na unyenyekevu na kwamba, Mitume walitambua Ukuu wa Mungu uliokuwa umejificha katika maisha ya mwanadamu na kwamba, ukweli ni mchakato unaowawezesha watu kukutana na hiki ni kiini cha ujumbe wa Kikristo. Ni mwaliko wa kutubu na kumwongokea Yesu Kristo, ambaye ni hazina kuu, inayomshirikisha mwanadamu furaha ya kweli na kwamba, Yesu Kristo anapaswa kuwa ni kiini cha maisha na utume wa Wakristo, kwa kutendeana mema.

Mchungaji Traettino anasema, kukutana na Yesu ni kukutana na ukweli ambao ni sehemu ya vinasaba vya Injili vinavyowawezesha Wakristo kuendeleza majadiliano ya kiekumene, ili wote waweze kuwa wamoja, kwa kujielekeza zaidi katika majadiliano ya kiekumene yanayobubujika kutoka katika maisha ya kiroho, ili kujenga umoja wa kweli kati ya watu wa mataifa sanjari na ujenzi wa Umoja wa Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Hapa kuna haja kwa wakristo kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu.

Fumbo la Umwilisho ni kielelezo cha hali ya juu kabisa cha upendo wa Mungu kwa binadamu; Mungu ambaye anajitambulisha kwa njia ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Wakristo wanaalikwa kuifia dhambi na ubinafsi wao, tayari kufufuka na kuvikwa taji ya utukufu na Roho Mtakatifu. Wakristo wanatumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu na kuwafunda watu kadiri ya Mafundisho ya Yesu.

Lengo ni kujenga na kuimarisha umoja katika imani, kwa kuonea aibu utengano, vita, madhulumu na kinzani hata nchini Italia. Pamoja na yote haya kuna haja kwa Wakristo kujielekeza zaidi na zaidi katika upatanisho, kanuni maadili, upendo, uwajibikaji kama ambavyo inajionesha kwa maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko.

Wakristo hawana budi kuwa ni kielelezo cha upatanisho unaobubujika kutoka katika undani wa maisha yao na kujidhihirisha kwa wao kujipatanisha na Yesu, ili kukumbatia Msalaba, kielelezo cha hali ya juu kabisa cha upendo wa Mungu kwa binadamu; upendo unaompatanisha binadamu na Muumba pamoja na jirani yake. Wakristo wa Kanisa la Kipentekoste wanamheshimu sana Mtakatifu Francisko wa Assis anayewachangamotisha kutafuta kwanza mambo msingi.







All the contents on this site are copyrighted ©.