2014-07-29 09:28:17

Roho Mtakatifu ni kielelezo cha umoja na utofauti wa karama ndani ya Kanisa!


Baba Mtakatifu Francisko anawahamasisha Wakristo kufanya hija ya pamoja wakiwa wameambatana na Yesu ambaye daima amejidhihirisha kuwa ni mvumilivu, hata pale wanapotenda dhambi, hakuna sababu ya kusimama wala kukata tamaa, bali wawe ni watu wenye matumaini. Yesu ni mwanga unaowaangazia waja wake katika hija ya maisha yao hapa duniani pamoja na kuwajalia nguvu ya kutembea salama.

Baba Mtakatifu ameyasema hayo, Jumatatu tarehe 28 Julai 2014 alipomtembelea rafiki yake Mchungaji Giovanni Traettino wa Kanisa la Kipentekoste kwenye Kanisa la Upatanisho ambalo bado linaendelea kujengwa huko Caserta, Tukio hili limehudhuriwa pia na umati wa waamini wa Kanisa la Kipentekoste kutoka ndani na nje ya Italia. Baba Mtakatifu anasema, katika mahangaiko ya kuganga njaa, watoto wa Yakobo walibahatika kukutana na ndugu yao Yosefu waliyekuwa wamemsaliti kwa kumuuza utumwani Misri.

Wakristo wanapaswa kutembea huku wakiwa wameshikamana ili kujenga na kudumisha umoja wa Kanisa, kwa kuvuka kikwazo cha chuki na uhasama mambo ambayo kwa sasa hayana tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo. Kazi kubwa inayotekelezwa na Shetani ni kupandikiza mbegu ya utengano kati ya Wakristo, lakini ikumbukwe kwamba, Yesu katika sala yake ya Kikuhani ameombea umoja wa Kanisa, hata katika utofauti wake, kazi ambayo inatekelezwa na Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anasema hapa kuna haja ya kujenga umoja uliopatanishwa na Roho Mtakatifu, kwa kuwawezesha Wakristo kushirikishana karama katika maelewano. Utandawazi ulichangamotishe Kanisa kushikamana kwa kuendelea kujikita katika taalimungu ya kiekumene mintarafu kazi ya Roho Mtakatifu sanjari na kutembea mbele ya Mwenyezi Mungu, ili kukutana na ndugu katika Kristo.

Baba Mtakatifu Francisko amegusia kuhusu Fumbo la Umwilisho, Neno wa Mungu alipofanyika mwili na kukaa kati ya watu wake. Yesu ni Mtu kweli na Mungu kweli, aliyezaliwa bila kuumbwa, Mwenye Umungu mmoja sawa na Baba, kielelezo cha upendo wa Mungu kwa binadamu na changamoto kwa binadamu kupendana wao kwa wao, lakini zaidi kwa kuonesha upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Wakristo wanahimizwa kwenda pembezoni mwa Jamii ili kuwatangazia watu Injili ya Furaha, kwani watu wana kiu na njaa ya kukutana na Mungu pamoja na kusikia ukweli kuhusu Yesu Kristo. Ikumbukwe kwamba, Injili ni kielelezo cha upendo, ukweli, uzuri na furaha. Wivu na chuki ni vikwazo katika kutangaza Injili ya Furaha na matokeo yake ni Wakristo kugawanyika na hata kudhulumiana kama ilivyojitokeza kwa baadhi ya Wakatoliki kuwanyanyasa Wakristo wa Makanisa ya Kipentekoste, kwani walionekana kuwa kama "kiwingu".

Baba Mtakatifu Francisko ametumia fursa hii kuomba msamaha kwa dhuluma na nyanyaso zilizofanywa na Wakatoliki dhidi ya Wakristo wa Kanisa la Kipentekoste. Anamwomba, Mwenyezi Mungu awakirimie ujasiri wa kutambua udhaifu huu na kuthubutu kuomba msamaha. Ukweli unawawezesha watu kukutana katika hija ya maisha kwa kumtafuta ili hatimaye kuweza kumkumbatia Yesu ambaye daima anawatangulia katika hija na mahangaiko yao ya ndani.

Baba Mtakatifu amewashukuru wenyeji wake kwa kumwezesha kukutana na Wakristo wa Kanisa la Kipentekoste na kushirikishana nao utajiri wa maisha na utume wa Kanisa, daima wakijitahidi kumwendea Yesu ambaye ndiye yule Mwanakondoo wa Mungu anayeondoa dhambi za dunia. Wafuasi wa kwanza waliokutana na Yesu, walibadilika na kuwa watu wapya zaidi, kiasi cha kuwa ni watakatifu wanaojikita katika umoja wa Kanisa. Wakristo waendelee kushirikiana katika umoja na mapendo kama ushuhuda wa majadiliano ya kiekumene yanayojikita katika uhalisia wa maisha!







All the contents on this site are copyrighted ©.