2014-07-29 11:52:05

Huu ni wakati wa kutenda kwa unyenyekevu, amani na utulivu wa ndani!


Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni alifanya mahojiano na gazeti moja linalochapishwa nchini Argentina, El Clarin, ili kuzungumzia mambo msingi yaliyojiri katika maisha na utume wake katika kipindi hiki tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki.

Kwa bahati mbaya kuna watu wengi wanadhani kwamba, siri ya furaha inajikita katika afya njema, upendo, mali, madaraka na mambo kama haya, lakini Baba Mtakatifu anasema, watu wanapaswa kuishi kadiri wanavyokirimiwa na Mwenyezi Mungu pasi na kutafuta makuu. Katika ujana wake, alikuwa bega kwa bega kumsaidia mama yake katika kazi za nyumbani na kwamba, alimsindikiza mama yake mzazi hata katika dakika zake za mwisho wa maisha yake, akiwa na furaha na utulivu wa ndani kutokana na kazi kubwa aliyoifanya katika maisha yake.

Baba Mtakatifu anasema, changamoto kubwa kwa watu wa kizazi hiki ni kuonesha upendo na mshikamano wa dhati kwa watu wanaotafuta nafuu katika maisha yao; watu wanaokimbia vita, nyanyaso, dhuluma na majanga asilia. Bara la Ulaya kwa sasa linawaogopa wahamiaji, lakini hata hivyo kuna nchi kama Uswiss ambayo hata katika udogo wake, imekuwa ni kielelezo cha upendo na mshikamano kwa kutoa hifadhi kwa wahamiaji laki nane.

Kuna tofauti kubwa kati ya watu wanaoishi Kaskazini na Kusini, kiasi kwamba, hakuna uwiano mzuri wa matumizi ya rasilimali ambayo kimsingi ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inayopaswa kutumiwa kwa ajili ya mafao ya wengi. Kuna idadi kubwa ya maskini wa hali na kipato katika nchi changa duniani, ingawa wana utajiri na rasilimali nyingi. Uchimbaji wa madini umekuwa ni chanzo kikubwa cha uchafuzi wa mazingira hali ambayo inasababisha majanga makubwa kwa watu!

Baba Mtakatifu anasema, katika maisha yake hajawahi kutamani mambo makubwa yanayozidi uwezo wake. Alipokuwa kijana alijiona kuwa ni mwamba thabiti na wakati wa ujana wake amekuwa kama ni mto unaotembea na katika uzee anajiona kwamba, kasi ya maji imepungua kwa kiasi kikubwa. Huu ni wakati wa kufanya kazi kwa unyenyekevu, uvumilivu, amani na utulivu!







All the contents on this site are copyrighted ©.