2014-07-28 11:23:31

Kamwe msikate tamaa!


Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Makanisa ya Mashariki, Jumapili tarehe 27 Julai 2014 ameadhimisha Ibada ya Liturujia ya Neno la Mungu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Diego, Calfornia, ili kusali kwa ajili ya kuwaombea Wakristo wanaoteseka huko Iraq, Syria, Palestina na Misri.

Wamewakumbuka pia wananchi wanaoteseka kutokana na vita huko Ukrain. Waamini wa Makanisa ya Mashariki wanamshukuru sana Baba Mtakatifu Francisko kwa kuonesha moyo wa upendo na mshikamano kwa Wakristo na wote wanaoteseka sehemu mbali mbali kutokana na dhuluma za kidini pamoja na vita. Kardinali Sandri amewapongeza Wakristo kwa kuendelea kuwa mashahidi wa imani na waaminifu kwa Injili ya Kristo hasa katika kipindi hiki kigumu cha maisha yao.

Waamini wanaendelea kuhamasishwa kushikamana kwa dhati na wote wanaoteseka kutokana na kulazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Waamini wasikate tamaa, bali waendelee pia kusali kwa ajili ya kuombea haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Ibada hii imehudhuriwa na viongozi na wakristo kutoka katika Makanisa ya Mashariki wanaoishi mjini Calfornia. Kardinali Sandri amekutana na kuzungumza pia na waamini wa Makanisa ya Mashariki kutoka Jijini Los Angeles na San Diago. Akiwa nchini Marekani anatarajia pia kuwatembelea na kuzungumza na Wakristo wa Makanisa ya Mashariki ili kwa pamoja kuweza kuangalia changamoto zinazojitokeza katika mikakati ya shughuli za kichungaji.







All the contents on this site are copyrighted ©.