2014-07-22 15:29:45

Ujumbe wa Papa kwa Siku ya Maisha Uingereza


(Vatican Radio)Kila mwaka tarehe 27 Julai, Kanisa Katoliki nchini Uingrereza na Ireland, husherekewa kama Siku ya Maisha, katika maana ya kuyapenda, kuyalinda na kuyatetea tangu mwanzo wake hadi hatma yake ya kawaida. Ni siku hasa inayowahusisha vijana, kuyajali na kuyatunza maisha kwa heshima kwenye kila hatua ya makuzi.

Kwa ajili ya siku hii, Papa Francisco, amepeleka ujumbe wake , uliotiwa sahihi na Katibu wa Vatican Kardinali Pietro Parolin, ambamo anatoa wito kwa watu wote wenye mapenzi mema, kuyafurahia maisha, hasa kwa namna ya kipekee katika kuwajali wale walio katika mazingira magumu na hatarishi.


Ujumbe huu uliotumwa kwa Kanisa Uingereza, Ireland, Scotland na Wales, unawataka Wakatoliki kupeleka upendo na huruma ya Kristo, kama majitoleo ya uzima, kwa wale wanao sumbuka na aina mpya ya umaskini na mazingira magumu, yanayozidi kujitokeza dhahiri katika jamii ya kisasa kama ilivyoelezwa katika Waraka wa Kitume wa Injili ya Furaha (cf. Evangelii Gaudium 210).


Mandhari ya mwaka huu kwa ajili ya Maisha ni Kuishi , Kulinda na kufurahia Maisha tangu mwanzo wake hadi mwisho wake wa asili. Kwao wote wanao husika na ufanikishaji wa Siku hii ya Maisha, Baba Mtakatifu Francisco amewapa Baraka zake za kichungaji, akiwatakia hekima, furaha na amani ya Bwana Mfufuka."







All the contents on this site are copyrighted ©.