2014-07-21 10:12:41

Taizè kuelekea Mwaka 2015!


Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè kuanzia tarehe 9 Julai hadi tarehe 16 Agosti 2015 itaadhimisha kilele cha Jubilee ya miaka 75 tangu kuzaliwa kwa Muasisi wake Fra Roger na miaka 10 tangu alipofariki dunia. Ni tukio linalotarajiwa kuwakutanisha vijana wa kiekumene kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wawakilishi wa dini na serikali pamoja na maskini na wale wanaohudumiwa na Jumuiya hii. RealAudioMP3

Mwezi Julai 2015, vijana wanaoishi katika Monasteri au katika nyumba za kitawa watashirikishwa ili kukutana na kuzungumza na wakuu wa mashirika ya kimonasteri na kitawa kutoka Makanisa ya Kiorthodox, Kikatoliki na Kiluteri. Kati ya viongozi mashuhuri wanaotarajiwa kuwepo ni pamoja na Padre Adolfo Nicolas, Mkuu wa Shirika la Wayesuit, Padre Bruno Cadorè, Mkuu wa Shirika la Wadomenikani pamoja na wakuu wa Mashirika ya Kitawa kwa upande wa wanawake.

Mwezi Septemba 2015 kutafanyika Kongamano la Kimataifa kuhusu mchango wa Frà Roger katika masuala ya kitaalimungu, tema itakayochambuliwa na Kardinali Walter Kasper, Rais mstaafu wa Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa umoja wa Wakristo. Hapa vijana waliobobea katika taalimungu watashiriki kikamilifu, ili kutoa mchango wao wa jinsi wanavyomfahamu Frà Roger.

Taarifa zinazonesha kwamba, kuanzia Mwezi Julai kuna mikutano muhimu inayoendelea kufanyika kwenye Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè. Kila Jumapili, vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanafika kwenye Makao makuu kwa muda wa juma zima, ili kusali na kutafakari kuhusu Neno la Mungu. Vijana wengi kutoka Italia wanatarajiwa kuhudhuria huko mwishoni mwa mwezi Julai hadi mwezi Agosti. Fra Alois ndiye anayewaongoza vijana hawa katika tafakari ya kina inayohimiza upendo na mshikamano wa kidugu kati ya watu.








All the contents on this site are copyrighted ©.