2014-07-19 08:59:47

Vitendo vya kigaidi vinabomoa na wala havijengi kamwe!


Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Chama cha Waisraeli wa Argentina kinachoadhimisha miaka ishirini tangu shambulizi la kigaidi lilipofanywa dhidi ya makao makuu ya chama hiki kunako tarehe 18 Julai 1994 anasema kwamba, vitendo vya kigaidi vinabomoa, havijengi wala kusaidia maendeleo ya binadamu. Katika shambulio hilo watu 85 walipoteza maisha na wengine 200 kupata majeraha makubwa.

Baba Mtakatifu anasema, anapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati na Jumuiya ya Waisraeli wa Argentina pamoja na wale wote walioguswa na madhara ya shambulio hili la kigaidi. Baba Mtakatifu anakumbuka kwa uchungu mkubwa jinsi ambavyo vitendo hivi vimekatisha maisha ya watu wasiokuwa na hatia; vimeharibu matumaini ya watu na kwamba, Buenos Aires inapaswa kuwalilia watoto wake kwa uchungu mkubwa. Matukio kama haya hayapaswi kusahaulika haraka kiasi hiki, kwani historia inapaswaiwasaidie watu kuboresha mahusiano yao ya kijamii.

Baba Mtakatifu anasema, kuna haja ya kuhakikisha kwamba, haki inatendeka. Baba Mtakatifu anahitimisha ujumbe wake kwa sala kwa ajili ya kuziombea roho za marehemu waliofariki dunia katika tukio hili pamoja na familia zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.