Jimbo Katoliki Daejeon, Korea ya Kusini ni chemchemi ya mashahidi wa imani
Baba Mtakatifu Francisko katika hija yake ya kitume nchini Korea katika maadhimisho
ya Siku ya sita ya Vijana Barani Asia inayoongozwa na kauli mbiu “Ondoka, uangaze,
kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa Bwana umekuzukia” atapata nafasi ya kuonja
ukarimu kutoka kwa waamini wa Jimbo Katoliki la Daejeon, lililoko Korea ya Kusini,
mahali ambako si maarufu sana kwa wengi, lakini hapa ndipo ambapo Baba Mtakatifu Francisko
amepaona na kuamua kupatembelea.
Askofu Lazaro
You Heung-sik wa Jimbo Katoliki Daejeon anasema mashahidi wengi wa Korea waliojisadaka
kwa ajili ya kushuhudia Injili wanatoka katika Jimbo hili. Anakumbuka alipokutana
na kuzungumza na Mtakatifu Yohane Paulo II kunako mwaka 1981 na kumwahidia kwamba,
atajitahidi kuwa Padre mwema kwa ajili ya sifa na utukufu wa Kanisa la Kristo, jambo
ambalo lilimvutia Papa Yohane Paulo II ambaye alimzawadia Rozari tatu na baadaye katika
ujumbe wake kwa Mapadre kwa mwaka ule, aliwataka Makleri kuwa kweli ni mfano wa kuigwa.
Askofu
Lazaro You Heung-sik anasema, katika barua aliyomwandikia Baba Mtakatifu Francisko
akimwomba kushiriki katika Kongamano la sita la Vijana Barani Asia alimwelezea umuhimu
wa Jimbo lake katika mchakato wa ushuhuda wa maisha miongoni mwa waamini kwani hapa
ni kisima na chemchemi ya maisha ya mashahidi wengi waliojisadaka kwa ajili ya kusimamia
kweli za Kiinjili. Hapa ni mahali ambapo, waamini walei wamejijenga na kujiimarisha
katika maisha na utume wa Kanisa kama ilivyokuwa kwa Kanisa la mwanzo mjini Yerusalemu.
Waamini wa Jimbo Katoliki Daejeon wanamshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa hii
aliyowakirimia, ili kumwonjesha Baba Mtakatifu ukarimu na ushuhuda wa maisha ya waamini
kutoka Korea. Kuanzia tarehe 10 hadi tarehe 17 Jimbo hili litakuwa ni mwenyeji wa
Siku ya Vijana Korea sanjari na Siku ya Vijana Barani Asia, Itakumbukwa kwamba, wakati
wa maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani mwaka 2013 iliyofanyika mjini Rio de Janeiro,
Brazil, Korea iliwakilishwa na kundi la vijana 350, hawa kweli wameendelea kuwa ni
Wamissionari miongoni mwa vijana wenzao. Wako tayari kutoka kimasomaso bila woga wala
makunyanzi kwa ajili ya kuhudumia.
Waamini na watu wenye mapenzi mema, walishangazwa
sana kusikia kwamba, Baba Mtakatifu Francisko amekubali mwaliko wa kuhudhuria maadhimisho
ya Siku ya sita ya Vijana Barani Asia, tukio ambalo kwa hakika litaacha kumbu kumbu
ya kudumu katika mioyo ya vijana, waamini na watu wenye mapenzi mema nchini Korea.
Huu ni mwaliko na changamoto ya kuendeleza pia majadiliano ya kidini na kiekumene
na waamini wa dini na madhehebu mbali mbali nchini Korea na Asia katika ujumla wake,
ili haki, amani, upendo na mshikamano wa kidugu miongoni mwa waamini uweze kutawala
na kudumishwa.
Ukristo nchini Korea ni matunda ya Mmissionari kutoka Asia
aliyefika nchini humo kunako mwaka 1794 na kukuta kwamba, kuna waamini elfu nne waliokuwa
wamebatizwa. Kufumuka kwa vita kati ya Korea ya Kaskazini na Korea ya Kusini kati
ya mwaka 1950 hadi mwaka 1953 kulisababisha madhulumu makubwa dhidi ya Wakristo kiasi
kwamba, watu wengi wakakata tamaa kutokana na vita pamoja na madhara yake ambayo bado
yanaendelea kuwatendea vibaya wananchi wa Korea zote mbili.
Maadhimisho ya
Siku ya sita Barani Asia yatakuwa ni jukwaa la Uinjilishaji, fursa ya majadiliano
ya kina na Baba Mtakatifu Francisko kwa heshima ya Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni,
Mama wa Kristo na Mama wa Kanisa.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.