2014-07-18 11:07:33

Sala kwa ajili ya kuombea amani Cameroon na maeneo yanayobaliwa na vita!


Askofu mkuu Samuel Kleda wa Jimbo kuu la Douala nchini Cameroon, ambaye pia ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Cameroon anasema, Jumamosi, tarehe 19 Julai 2014 ni siku ya kuombea amani nchini Cameroon na maeneo ambayo yanakabiliwa na vita kwa wakati huu. Kanisa linapenda kuwahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini Cameroon kutambua hatari kubwa iliyoko mbele yao inayofichika katika mashambulizi ya kigaidi yanayofanywa na Kikundi cha Boko Haram kutoka Nigeria, kwenye maeneo yaliyoko Kaskazini mwa Cameroon.

Jumamosi, waamini na watu wote wenye mapenzi mema wataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na kufanya maandamano kwa ajili ya kuombea amani, utulivu na ustawi nchini Cameroon pamoja na kuomba tunza na ulinzi kutoka kwa Mwenyezi Mungu dhidi ya mashambulizi ya kigaidi yanayotishia usalama wa watu na mali zao. Mashambulizi haya ni tishio kwa mshikamano wa kitaifa kati ya waamini wa dini ya Kiislam na Kikristo, kumbe kuna haja ya kushirikiana kwa pamoja, ili kupinga na kudhibiti vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na Boko Haram.







All the contents on this site are copyrighted ©.