2014-07-18 15:20:33

Papa azungumza kwa njia ya simu na Rais Peres na Rais Abbas!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa asubuhi tarehe 18 Julai 2014 amempigia simu Rais Peres Shimon wa Israeli na Mahmoud Abbas wa Palestina ili kuwaelezea masikitiko yake makubwa kutokana na mashambulizi yanayoendelea kwenye Ukanda wa Ghaza, hali ambayo inachochea na kuendeleza uhasama kati ya wananchi wa mataifa haya mawili pamoja na kusababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao. Kutokana na mashambulizi hayo, watu wengi wanateseka sana na kwamba, wanahitaji msaada kutoka katika Jumuiya ya Kimataifa.

Mazungumzo ya simu kati ya Baba Mtakatifu Francisko na Marais wa Israeli na Palestina ni mwendelezo wa juhudi zake za makusudi kwa ajili ya kuombea amani huko Mashariki ya Kati kama alivyofanya, Jumapili tarehe 13 Julai 2014 wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana. Baba Mtakatifu bado anakumbuka moyoni mwake, hija yake ya kichungaji aliyoifanya Nchi Takatifu pamoja na ule mkutano kwa ajili ya kuombea amani Mashariki ya Kati, uliowakutanisha viongozi kutoka Israeli na Palestina mjini Vatican hapo tarehe 8 Juni 2014.

Katika mazungumzo yake, Baba Mtakatifu amewahakikishia Marais hawa sala za Kanisa kutoka sehemu mbali mbali za dunia kwa ajili ya kuombea amani katika Nchi Takatifu. Hawa ni watu wa amani, wanataka amani na wataendelea kuombea amani hadi pale amani ya kweli itakapopatikana huko Mashariki ya Kati.

Amewakumbusha viongozi wa kitaifa na kimataifa kwamba, wanadhamana nyeti ya kulinda na kudumisha amani kwa kusitisha chuki, kinzani na uhasama kati ya Waisraeli na Wapalestina, ili kutoa fursa kwa mchakato utakaositisha vita, ili amani na upatanisho vianze tena kuchipuka kutoka katika mioyo ya watu!







All the contents on this site are copyrighted ©.