2014-07-18 08:41:24

Mshikamano na Kanisa Barani Afrika!


Tume ya Afrika ya Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, USCCB, imeidhinisha kiasi cha dolla za Kimarekani millioni 1. 3 kwa ajili ya kugharimia miradi arobaini na sita kwa ajili ya Kanisa Barani Afrika. Maamuzi haya yamefanywa na Maaskofu Katoliki Marekani katika mkutano wao uliofanyika hivi karibuni huko New Orleans. RealAudioMP3

Kanisa Barani Afrika linaendelea kukua na kupanuka kwa kasi ya ajabu na kwamba linakabiliwa na changamoto mbali mbali katika kuzima kiu ya maendeleo ya watu wanaowazunguka, anasema Kardinali Theodore McCarrick, Askofu mkuu mstaafu wa Jimbo kuu la Washington DC, ambaye kwa sasa ni Mwenyekiti wa Tume ya Afrika ya Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani.

Msaada huu unalenga kuliwezesha Kanisa Barani Afrika kuweza kuandaa rasilimali watu ili kutekeleza kazi ya Uinjilishaji mpya kwa kuwa na utaalam na ujuzi unaohitajika ili kuongeza tija na ubora wa shughuli za kichungaji. Pili ni kuendelea kulisaidia Kanisa Barani Afrika kujenga uwezo ili hatimaye, liweze kujitegemea na kujiendesha lenyewe kwa kutumia kikamilifu rasilimali watu na vitu vilivyoko Barani Afrika kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika na watu wake kwa ujumla. Hapa kuna haja ya kuwaandaa viongozi wanaoweza kujisadaka na kujitosa kwa ajili ya Kanisa la Bara la Afrika.

Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani litaendelea kushirikiana na Kanisa Barani Afrika ili kufikia malengo yaliyobainishwa na pande hizi mbili. Taarifa zinaonesha kwamba, Baraza la Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, limepewa msaada wa dolla za kimarekani 30, 000 ili kusaidia majiundo makini ya viongozi, gharama za uendeshaji pamoja na mikakati ya haki na amani. Wanawake kutoka Afrika ya Kusini, Bostwana na Swaziland wanatarajiwa kunufaika na msaada huu.

Kiasi cha dolla za kimarekani 25, 000 zimetolewa kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Ethiopia kama sehemu ya mchakato wa kumwilisha utekelezaji wa Waraka wa Kichungaji wa Baba Mtakatifu Francisko, Injili ya Furaha, “Evangelii gaudium” katika lugha ya taifa. Fedha hii itagharimia mafunzo kwa viongozi wa kitaifa ambao baadaye watashirikisha mang’amuzi yao katika ngazi za Kijimbo na Kiparokia.

Kardinali Theodore McCarrick anasema, msaada unaotolewa na Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani unalenga kuliwezesha Kanisa Barani Afrika kutekeleza utume wake hasa miongoni mwa Maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko. Msaada unaotolewa kwa Kanisa Barani Afrika ni sehemu ya Mfuko wa mshikamano kutoka katika Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani.








All the contents on this site are copyrighted ©.