Ilikuwa ni tarehe 21 Novemba 1964 Mtumishi wa Mungu Papa Paulo wa VI alipotia mkwaju
Waraka wa Kichungaji kuhusu Majadiliano ya Kiekumene "Unitatis Redintegratio", matunda
ya maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Kama sehemu ya maandalizi ya tukio
hili muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa, Baraza la Maaskofu Katoliki Canada,
limewaandikia waamini na watu wote wenye mapenzi mema Ujumbe wa maadhimisho ya Jubilee
ya Miaka 50 ya mchakato wa Umoja wa Wakristo.
Maaskofu wanasema umoja miongoni
mwa Wakristo ni changamoto endelevu inayopaswa kufanyiwa kazi na Wakristo wote, kwani
hili ni agizo la Kristo mwenyewe ili wote wawe wamoja. Katika kipindi cha miaka hamsini
iliyopita, Kanisa limepiga hatua kubwa ya majadiliano ya kiekumene na Makanisa ya
Kikristo, hii ni njia iliyoanzishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.
Wakristo wamepiga hatua kubwa kwa kufahamiana na kushirikiana kwa pamoja kama ushuhuda
wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Ni katika mchakato huu, Baraza la Maaskofu
Katoliki Canada, kunako mwaka 1965 likaanzisha Tume ya Majadiliano ya Kiekumene na
Kidini. Malengo makuu ya tume yalikuwa ni kuanzisha mahusiano na Makanisa ya Kikristo
nchini Canada; kuwa ni mahali pa kufanya rejea katika mikakati ya majadiliano ya kidini
na kiekuemene pamoja na kuhamasisha majadiliano ya kiekumene katika ngazi ya ktaifa.
Kunako mwaka 1998, Tume hii ikawa na hadhi ya Baraza la Kiekumene kama yalivyo
kwa Makanisa mengine nchini Canada. Katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita, kumekuwepo
na maendeleo makubwa katika kukuza na kudumisha mahusiano ya kiekumene kati ya Makanisa
ya Kikristo. Ni mahusiano yanayojikita katika maisha ya: Sala, ushuhuda na ukarimu
wa wafuasi wa Kristo.
Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Majadiliano ya
Kiekumene, iwe ni fursa kwa Wakristo kushikamana zaidi kwa kuwa wamoja ndani ya Kristo
sanjari na kuendelea kupandikiza mbegu ya imani, unyenyekevu, uvumilivu, toba na msamaha
ili kuponya madonda ya utengano yaliyojitokeza ndani ya Kanisa.
Baraza la
Maaskofu Katoliki Canada kwa namna ya pekee, linakumbuka tukio la kihistoria lililowakutanisha
Baba Mtakatifu Francisko na Patriaki Bartolomeo wa kwanza wa Kanisa la Kiorthodox
la Costantinopoli mjini Yerusalemu wakati wa kumbu kumbu ya Jubilee ya miaka 50 tangu
Papa Paulo wa VI na Patriaki Anathegoras walipokutana kusali pamoja. Baraza la Maaskofu
Katoliki Canada linawahimiza waamini kama mtu binafsi na Jumuiya kujikita katika kuhamasisha
umoja na mshikamano miongoni mwa Wakristo, kwa kuanzia katika familia, shule na Parokia
mbali mbali! Wakristo wote wajisikie kuwa wamoja ndani ya Kristo!