Maadhimisho ya Mkutano mkuu wa kumi na nane wa AMECEA, yalianza rasmi hapo tarehe
16 Julai 2014 kwa mafungo yaliyoongozwa na Askofu mkuu Yuda Thaddeus Ruwaichi wa Jimbo
kuu la Mwanza, aliyekazia umoja, upendo na mshikamano miongoni mwa Familia ya Mungu
katika nchi za AMECEA.
Jioni wajumbe walitafakari kuhusu moyo, mwono, utume
na tunu msingi zinazoongoza AMECEA, mada iliyowakilishwa na Kardinali John Njue, Askofu
mkuu wa Jimbo kuu la Nairobi pamoja na Padre Pius Rutechura, Makamu mkuu wa Chuo Kikuu
cha Kikatoliki Afrika Mashariki na Kati, CUEA.
Alipowasili mjini Lilongwe,
Malawi, Kardinali Njue akizungumza na waandishi wa habari alisema kwamba, Kanisa Barani
Afrika halina budi kujipanga vyema ili kuhakikisha kwamba, linajitegemea na kujiendeleza
ili kuachana na kasumba ya kuendelea kutegemea misaada kutoka kwa wafadhili ng'ambo,
utamaduni ambao kwa sasa umepitwa na wakati.
Ni jukumu la Maaskofu Katoliki
kutoka AMECEA kuwahamasisha waamini wao ili waweze kujitegemea, kwa kuwajengea uwezo
mihimili mikuu ya Uinjilishaji, ili iweze kweli kutekeleza dhamana na wajibu wake
msingi. Mbegu ya imani iliyopandikizwa kwa sadaka kubwa ya wamissionari inapaswa kukuzwa
na kudumishwa, ili kuweza kuzaa matunda yanayokusudiwa.
Maadhimisho ya mikutano
ya AMECEA ni fursa ya kusali, kutafakari na kushirikishana mang'amuzi na vipaumbele
katika maisha na utume wa Kanisa Barani Afrika. Lengo ni kuhakikisha kwamba, AMECEA
inairithisha Familia ya Mungu tunu msingi za maisha ya kiroho, kimaadili na kiutu.
Kwa namna ya pekee, amewashukuru na kuwapongeza waamini na wananchi wa Malawi kwa
mapokezi makubwa waliowaonesha wajumbe wa AMECEA walipokuwa wanawasili nchini humo
kwa mkutano wao.