2014-07-17 09:04:47

Mikakati ya kulinda na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia!


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika ya Kati, ACERAC, limehitimisha mkutano wake mkuu ulioanza huko Brazzaville, Congo kuanzia tarehe 6 hadi tarehe 13 Julai 2014 kwa kupitisha maazimio ishirini na matatu yatakayofanyiwa kazi na Familia ya Mungu Afrika ya Kati, katika mchakato wa kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya Familia inayojikita katika mahusiano ya kudumu kati ya Bwana na Bibi. RealAudioMP3

Maaskofu wanasema, Familia inakabiliwa na changamoto nyingi katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia sanjari na mabadiliko msingi katika maisha ya kijamii, kitamaduni na kiuchumi; mambo yanayochangia kushamiri kwa ubinafsi, ubabe na anasa. Maaskofu wanabainisha kwamba, hivi ni vishawishi ambavyo kimsingi vinasigana sana na tunu msingi za maisha ya kifamilia kadiri ya mapokeo na tamaduni njema za Kiafrika; yaani ile hali ya mtu kujitosa kisawasawa katika upendo!

Maaskofu wanakazia umuhimu wa kufanya maandalizi ya kina kwa wanandoa watarajiwa, ili kuweza kukabiliana na changamoto za maisha ya ndoa na familia, jambo ambalo linahitaji mikakati makini ya kichungaji kuhusu utume wa familia. Maaskofu wanawataka waamini waliopewa dhamana katika tume ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya familia kuhakikisha kwamba, zinatekeleza dhamana na wajibu wake bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Familia Barani Afrika.

Hapa mihimili ya Uinjilishaji yaani: Mapadre, Watawa na Makatekista, wanapaswa kufundwa barabara, ili waweze kuimarisha na kuendeleza mafundisho ya Kanisa kuhusu ndoa na familia. Wanandoa wapya wasindikizwe katika safari ya maisha yao ya unyumba hatua kwa hatua, kwa kutambua kwamba, maisha ya unyumba si maji kwa glasi yataka moyo kweli kweli! Wanandoa wafundishwe kuhusu utu na heshima ya binadamu, wajitambue na kujitahidi kufahamiana kikamilifu, ili kusaidiana katika hija ya maisha ya ndoa na familia.

Wanandoa wafundishwe tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kadiri ya Mafundisho ya Kanisa, ili kupamba maisha yao ya ndoa kwa manukato ya tunu msingi za Kikristo. Wanandoa wahamasishwe kusoma, kulitafakari na kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha; wajifunze kanuni maadili na maisha ya imani, ambayo kimsingi yanachambuliwa kwa kina na mapana katika Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki na Muhtasari wa Mafundisho Jamii ya Kanisa.

Maaskofu wanawahimiza wazazi na walezi kujitaabisha katika kuwapatia watoto wao elimu na malezi bora ya maisha ya Kikristo, kimaadili na kitamaduni kwa kutambua kwamba, familia ni shule ya kwanza ya imani, maadili na utu wema. Hapa ni mahali ambapo watoto wanajifunza kujiheshimu na kuheshimiana. Vijana wafundwe kutekeleza wajibu wao kikamilifu katika maisha ya kijamii na kikanisa; kwa kupenda kufanya kazi kwa juhudi na maarifa, ili kutumia vyema nguvu walizojaliwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ustawi na maendeleo yao na Jamii inayowazunguka.

Familia za Kikristo zinahamasishwa kutolea ushuhuda wa maisha yao kwa njia ya imani tendaji kama njia ya kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya. Wanafamilia washiriki kikamilifu katika maisha ya kijamii, kisiasa na kiuchumi, ili kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya chachu ya utakatifu wa maisha.

Maaskofu Katoliki Afrika ya Kati wanawakumbusha waamini kwamba, maisha ya Kikristo yanasimikwa katika nguzo kuu nne yaani: Neno la Mungu, Maisha ya Kisakaramenti, hasa Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Sakramenti ya Upatanisho, Sala binafsi pamoja na Sala za Kifamilia. Wanandoa wajenge utamaduni wa mawasiliano yanajikita katika ukweli, uwazi, amani na upendo katika familia. Wajenge utamaduni wa kufanya tathmini ya maisha yao mara kwa mara kwa kuona wapi walipopiga hatua na wapi ambapo kama familia wametindikiwa ili waweze kuwa na ujasiri wa kuomba “divai” kwa Yesu kupitia kwa Bikira Maria. Hapa lengo ni kujenga na kukuza utamaduni wa wongofu wa ndani, toba na msamaha katika maisha ya waamini.

Maaskofu wanaendelea kuhimiza umuhimu wa familia za Kikristo kuheshimiana, kupendana na kusaidiana; kwa kuheshimu na kuthamini utu na heshima ya wanawake kwani hata wao wana mchango mkubwa. Hii ni changamoto ya kuondokana na mfumo dume unaotaka kuwakandamiza na kuwanyanyasa wanawake na wasichana; hizi ni mila, desturi na tamaduni ambazo zimepitwa na wakati.

Bado kuna changamoto kubwa katika kukuza na kuendeleza ndoa mseto, hapa wanandoa hawa wanapaswa kusaidiwa kikamilifu katika kutoa malezi na majiundo makini kwa watoto wao. Tatizo kubwa wanakiri Maaskofu ni misimamo mikali ya kiimani inayoendelea kujengeka kwa kasi kubwa Barani Afrika.

Maaskofu wanawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuachana na mila na desturi zinazoendekeza uchawi na imani za kishirikina kwani mambo haya ni kati ya sababu kubwa zinazopelekea uvunjifu wa misingi ya haki na amani, mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, kwa maneno machache ni mila na desturi zinazoendeleza utamaduni wa kifo! Waamini wajifunze na wawe waadilifu katika kutumia njia za mawasiliano ya kijamii, kwa ajili ya kujenga na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia na wala si kubomoa maadili na utu wema.
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Afrika ya kati, ACERAC linahimiza mikakati ya kichungaji inayojikita katika upendo na mshikamano kwa ajili ya kuzisaidia familia ambazo zinajaribiwa na athari za myumbo wa uchumi kimataifa na kitaifa; kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi pamoja na kuanza mchakato wa kuandika Mwongozo wa wa Katekesi kuhusu Familia, itakayodumu kwa muda wa miaka mitatu. Matatizo na changamoto zinazoendelea kuiandama taasisi ya familia, iwe ni fursa ya kushirikiana kikamilifu na Roho Mtakatifu katika kukuza na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya!

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.