2014-07-17 10:49:39

Chakarikeni kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika!


Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki hivi karibuni akichangia mada kwenye kongamano la kimataifa lililokuwa limeandaliwa na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu katoliki Afrika na Madagascar SECAM kwa kuongozwa na kauli mbiu “Kanisa Barani Afrika: kutoka Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican hadi mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo: mchango wa Papa Yohane XXIII na Yohane Paulo II.” anasema umefika wakati kwa Familia ya Mungu Barani Afrika kujishughulisha na ustawi na maendeleo yake mwenyewe kwa kuangalia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. RealAudioMP3

Umefika wakati kwa wananchi barani Afrika kujifunga kibwebwe kupambana kufa na kupona na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, ili kujipatia maendeleo ya kweli. Kwa njia hii Bara la Afrika litaweza kutoka kifua mbele kulinda na kudumisha utu na heshima yake kwa kuwajibika barabara.

Bara la Afrika lisipoibua sera na mikakati bora ya maendeleo na ustawi wa watu wake, litaendelea kudharauriwa na kunyanyaswa na mataifa yanayotoa misaada kwa Bara la Afrika. Kwa sasa kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa, inaonekana kana kwamba, nchi wahisani zimechoka kuendelea kubeba “zigo” la misaada kwa Bara la Afrika. Hii ndiyo hali halisi inayojionesha kwa sasa kwani mwenye macho haambiwi atazame mwenyewe!

Kardinali Robert Sarah ambaye aliwahi kuwa ni Rais wa kwanza wa SECAM amewataka Waafrika ndani na nje ya Bara la Afrika kujielekeza zaidi na zaidi katika kutafuta ujuzi na maarifa; rasilimali watu, fedha na vitu kwa ajili ya kuendeleza Bara la Afrika, jambo linalohitaji moyo wa uzalendo, upendo na mshikamano badala ya watu kujikita katika ubinafsi, uchu wa mali na madaraka, mambo ambayo yameendelea kulitumbukiza Bara la Afrika katika mkwamo wa maendeleo. Dhana ya Bara la Afrika kuendelea kutegemea misaada kutoka ng’ambo imepitwa na wakati, sasa Afrika inapaswa kuwajibika kwa ajili ya maendeleo yake.

Kardinali Sarah anasema, hadi pale Familia ya Mungu Barani Afrika itakapokuwa na uchungu pamoja na usongo wa maendeleo yake, hapo Afrika itaweza kucharuka kwa maendeleo. Bara la Afrika linahitaji miundo mbinu itakayojikita katika masuala ya watu na tamaduni pamoja na imani zao. Kuna haja ya kujenga mfumo wa maendeleo endelevu unaowajibisha na kujenga umoja na udugu pamoja na kuimarisha uchumi unaosimikwa katika haki inayoshughulikia mafao ya wengi, kuliko hali ya sasa rasilimali na uchumi ni kwa ajili ya watu wachache, lakini “akina yakhe pangu pakavu weka mchuzi” wanaendelea kuogelea katika umaskini wa hali na kipato!

Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani anasema, maadhimisho ya Sinodi mbili za Maaskofu wa Afrika zimeleta mwamko mpya kwa maisha na ustawi na maendeleo ya Familia ya Mungu Barani Afrika. Changamoto kubwa iliyoko mbele ya Kanisa Barani Afrika ni kuhakikisha kwamba, linatekeleza mashauri ya kitume yaliyotolewa na Papa Yohane Paulo II na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI.

Maadhimisho ya Sinodi ya kwanza ya Maaskofu wa Afrika yaligubikwa furaha na huzuni. Kilikuwa ni kipindi cha kuporomoka kwa sera za ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini, lakini Afrika ikajikuta inatumbukia katika majonzi makubwa kutokana na mauaji ya kimbari yaliyokuwa yanatendeka nchini Rwanda. Kwa sasa Bara la Afrika linahitaji anasema Kardinali Peter Turkson kujielekeza zaidi katika misingi ya haki, amani na upatanisho kutoka ndani na nje ya Bara la Afrika.

Kwa upande wake Professa Albert Tevoedjre, Rais wa Mfuko wa Kardinali Bernadin Gantin, nchini Benin anasema, dunia inaweza kuokolewa kutoka kwenye mahangamizi na utepetevu wa misingi ya maadili na utu wema kwa kukumbatia na kuenzi tunu msingi za maisha bora ya kifamilia. Jambo hili linawezekana ikiwa kama familia zinazingatia misingi ya maadili na utu wema.

Bara la Afrika linaendelea kushuhudia kumong’onyoka kwa maadili na msingi bora ya maisha ya familia na ndoa, Familia ya Mungu Barani Afrika haina budi kukataa mielekeo inayotaka kuyumbisha tunu bora za maisha ya ndoa na familia kwa madai ya uhuru na demokrasia.

Waamini walei hawana budi kujengewa uwezo makini wa kupambana na mazingira yao kwa njia ya elimu pamoja na kuwawezesha vijana kuwa na dhamiri nyofu za kuweza kupambanua mema na mabaya badala ya mtindo wa sasa wa kuokota na kumeza kila kitu kinachooneshwa kwenye vyombo vya mawasiliano ya jamii. Kanisa Barani Afrika lazima liwekeze katika tunu msingi za maisha ya familia na vijana, ili waamini walei waweze kuwa ni chachu ya kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya kweli za Kiinjili, maadili na utu wema.

Kama walivyowahi kukazia Mababa wa awamu ya pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika kuna haja ya kuwapatia wanasiasa majiundo makini yatakayowasaidia kusimamia utu na heshima ya binadamu, mafao ya wengi na ustawi wa jamii. Mikakati hii haina budi kwenda sanjari na majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali, ili kwa pamoja waweze kujikita katika maendeleo na mafao ya wengi badala ya mwelekeo wa sasa unaowagawa wananchi kwa misingi ya udini, jambo ambalo ni sumu kali kabisa katika kukuza na kudumisha haki, amani na mafao ya wengi. Kinzani na migogoro ya kidini haina mashiko wala mafao kwa ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika.

Wanawake Barani Afrika wakiwezeshwa kielimu, kiuchumi na kisiasa wanaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika. Wanawake wanapaswa kuheshimiwa na kupewa nafasi ya kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa pamoja na kukoleza malezi na maendeleo ya jamii husika. Wanawake washirikishwe katika mchakato wa Uinjilishaji mpya, dhamana inayovaliwa njuga na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Wanawake washirikishwe katika vikao vinavyotoa maamuzi na kwamba, mfumo dume, nyanyaso na dhuluma kwa wanawake ni mambo ambayo hayana nafasi tena kwa Familia ya Mungu Barani Afrika.

Kongamano hili limeonesha kwa namna ya pekee mchango uliotolewa na Mtakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II katika maisha na utume wa Kanisa Barani Afrika. Ni viongozi hawa waliothubutu kwa mara ya kwanza katika historia ya Kanisa Katoliki kuteuwa viongozi wazalendo kutoka Barani Afrika kama: Makardinali, Maaskofu na viongozi waandamizi ndani ya Kanisa la Kiulimwengu, jambo ambalo lilikuwa kama ndoto kabla ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II ni viongozi wa Kanisa waliosimama kidete katika maendeleo ya Bara la Afrika, wanapaswa kukumbukwa kwa kumwlisha mafundisho yao katika uhalisia wa maisha na utume wa Kanisa Barani Afrika.

Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.