Rushwa, biashara haramu ya binadamu na dawa za kulevya ni majanga ya kimataifa!
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, akiwa nchini Mexico kuanzia tarehe
14- 15 Julai 2014 amekutana na kuzungumza na Rais Enrique Pena Nieto wa Mexico pamoja
na vyombo vya upashanaji habari nchini Mexico kwa kukazia dhamana na utume wa Kanisa
Katoliki nchini Mexico kuwa ni kuwasaidia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii ili kuweza kujikomboa kutokana na hali hii pamoja na kuendelea kushirikiana
na serikali katika mapambano dhidi ya matumizi haramu ya dawa za kulevya.
Itakumbukwa
kwamba, Kardinali Parolin alikuwa nchini Mexico kushiriki katika semina iliyokuwa
inajadili kuhusiana na mikakati ya kuratibu tatizo la wahamiaji nchini Mexico.
Kardinali
Parolin anabainishwa kwamba, sera na mikakati ya kichungaji inayotekelezwa na Mama
Kanisa inalenga kwanza kabisa kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu kwa kuzingatia
haki zake msingi. Ameipongeza Mexico kwa mabadiliko makubwa inayofanya kwenye Miundo
mbinu, Katiba, Sera na mikakati kwa ajili ya kulinda na kutetea haki msingi za wahamiaji
nchini Mexico. Kardinali Parolin ameishukuru pia serikali ya Mexico kwa jitihada hizi
zinazozingatia utu na heshima ya binadamu, hasa kwa wahamiaji ambao wanapata hifadhi
katika vituo vyake vilivyoenea sehemu mbali mbali nchini humo. Kanisa kwa upande wake,
litaendelea kutekeleza dhamana yake kama Msamaria mwema.
Kardinali Parolin
ameyasema yote haya wakati wa hafla ya chakula cha usiku kilichoandaliwa kwa niaba
yake na Rais Pena Nieto wa Mexico. Akizungumza na waandishi wa habari amekumbushia
kwa mara nyingine tena kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya umaskini na dhama ya uhamiaji
ambayo kwa sasa ni changamoto kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa, changamoto inayopaswa
kushughulikiwa kwa njia ya mshikamano wa kimataifa. Utengano wa kifamilia na wimbi
kubwa la watoto wanaojikuta wanalazimika kuhama nchi zao bila ya kusindikizwa na wazazi
au walezi wao ni jambo linalohatarisha usalama na maisha ya watoto hawa.
Kardinali
Parolin amegusia pia saratani ya rushwa, biashara haramu ya binadamu na dawa za kulevya,
majanga yanayomwandama mwanadamu katika ulimwengu mamboleo. Jambo la msingi ni vijana
kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima yao na kamwe wasikubali wajanja
wachache wawapokonye matumaini waliyo nayo kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko.
Kardinali
Pietro Parolin anasema katika ulimwengu wa utandawazi changamoto zote hizi zinapaswa
kushughulikiwa kwa pamoja na hakuna nchi inayoweza kujidai kwamba, inaweza kudhibiti
majanga haya kwa nguvu na jeuri yake peke yake. Hapa kuna haja ya kuwa na mikakati
pamoja na sera za pamoja kwa Bara la Amerika na katika Jumuiya ya Kimataifa kwa kutoa
kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu!