2014-07-15 10:25:45

Wahamiaji ni changamoto ya kimataifa!


Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa washiriki wa semina kuhusu wahamiaji iliyoandaliwa kati ya Mexico na Vatican kuanzia tarehe 14 -15 Julai, 2014 anasema kwamba, uhamiaji ni kati ya changamoto kubwa zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi, lakini bado haujapewa kipaumbele cha pekee na matokeo yake changamoto hii imekuwa ikifanyiwa mipango ya dharura.

Uhamiaji ni dhana inayofumbata matumaini na changamoto nyingi. Maelfu ya watu wanaolazimika kuzikimbia au kuzihama nchi zao wanajikuta wakikabiliana na kifo, haki zao msingi haziheshimiwi wanajikuta wakiwa wametengana na familia zao pamoja na kubaguliwa!

Baba Mtakatifu anasema kuna haja ya kuwa na mwelekeo mpya kuhusiana na suala ya wahamiaji kwa kuondokana na woga usiokuwa na mashiko, hali ya kutojali na kuwathamini wahamiaji, mambo yanayopelekea utamaduni wa utandawazi usiojali wa kuguswa na mahangaiko ya wengine. Hapa kuna haja ya kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kukutana, ili kujenga ulimwengu bora zaidi unaosimikwa katika misingi ya haki na udugu.

Baba Mtakatifu anawalika wahusika kuangalia tatizo la watoto wanaolazimika kuzikimbia nchi zao pasi na msaada wa wazazi au walezi wao kutokana na vita na umaskini, hili ni tatizo sugu linalojionesha kwa namna ya pekee na wahamiaji kutoka Amerika ya Kati na Mexico kuelekea mpakani mwa Marekani, ambako wanadhani kuna matumaini ya maisha, lakini ukweli wa mambo ni kwamba, wanateseka bure!

Watoto hawa wanapaswa kupokelewa na kutunzwa kwa kusaidiwa na sera makini na taarifa kuhusiana na hatari wanazoweza kukumbana nazo watoto hao zitolewe kwa usahihi. Jambo la msingi ni kuwa na sera makini za maendeleo katika nchi husika na kwamba, Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuwajibika kikamilifu katika kukabiliana na changamoto za uhamiaji.







All the contents on this site are copyrighted ©.