2014-07-15 12:22:29

Sisi sote ni familia moja mbele ya Mungu!


Baraza la Maaskofu Katoliki Japan limeadhimisha Siku ya Mabaharia Duniani, hapo tarehe 13 Julai 2014 kwa kukumbusha kwamba, majanga mbali mbali yanayoendelea kujitokeza huko baharini madhara yake yanajionesha sehemu mbali mbali za dunia, kumbe, kwa njia ya bahari, binadamu wote wanajikuta kuwa ni Familia moja inayopaswa kuoneshana upendo na mshikamano.

Katika ulimwengu wa utandawazi, haitoshi kufikiri na kutenda katika dhana hii, bali kwenda zaidi kwa kujikita katika mshikamano wa upendo, changamoto endelevu inayotolewa na Mama Kanisa kwa njia ya Maandiko Matakatifu. Kila mtu ashirikishwe katika mshikamano huu na kamwe hasiwepo mtu anayetengwa. Mabaharia na wavuvi wanapoondoka majumbani mwao ili kuendelea na shughuli zao wanafutika machoni pa wengi, hata kama wao ndio usukani muhimu katika mchakato wa uchumi na maendeleo ya binadamu.

Inasikitisha kuona kwamba, watu hawa wanasahaulika mapema na ni watu wachache sana wanaweza kuwakumbuka na kuwaombea katika shida na mahangaiko yao wanapokuwa kazini. Hata wakati mwingine, inawawia watu wengi kuwapatia msaada wa hali na mali. Ikumbukwe kwamba, binadamu wote mbele ya Mwenyezi Mungu ni Familia moja! Hii ni changamoto ya kuwakumbuka na kuwaombea mabaharia na wavuvi ili waweze kutekeleza majukumu yao na kurudi salama salimini ili waweze kuungana na familia zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.