2014-07-14 10:50:04

Udhaifu wa mwili!


Familia ya Chuo kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu pamoja na Hospitali ya Agostino Gemelli imemtumia Baba Mtakatifu Francisko salam na matashi mema kwa kuwatumia ujumbe kwa njia ya video, kuelezea masikitiko yake kwa kutoweza kuhudhuria katika kilele cha maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Kitivo cha Tiba na Upasuaji cha Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu.

Uongozi wa Hospitali ya Gemelli unamshukuru Baba Mtakatifu kwa kuwatia moyo wagonjwa na wote wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya tafiti na huduma kwa wagonjwa. Ni matumaini yao kwamba, wataweza kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu mapema iwezekanavyo!

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake anawakumbuka wote ambao kwa sasa wameanza likizo ya kipindi cha kiangazi, fursa makini ya kuweza kusali zaidi, kutafakari na kujipumzisha. Hiki ni kipindi kigumu kwa wazee na wagonjwa wanaojikuta wakiwa mamebaki pweke. Lakini kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu anawakumbuka wagonjwa waliolazwa kwenye Hospitali ya Gemelli, ambao hapo tarehe 27 Juni 2014 wakati wa Siku kuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu alitarajiwa kuwatembelea na kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili yao, lakini kutokana na afya yake kudorora dakika za mwisho akashindwa kutekeleza azma ya moyo wake.

Baba Mtakatifu anasema anatambua mateso waliyoyapata wote waliokuwa wamejitaabisha kwa ajili ya kuandaa tukio hili la kihistoria, lakini zaidi wagonjwa waliotamani kusali pamoja naye katika Ibada ya Misa Takatifu pamoja na kusalimiana nao ana kwa ana. Anawakumbuka wafanyakazi wote wa Hospitali ya Gemelli wanaotekeleza huduma kwa wagonjwa waliolazwa Hospitalini hapo, kuendelea kutekeleza wajibu huu kwa kutambua kwamba, Mungu peke yake ndiye nguvu yao, changamoto ya kutambua na kuthamini umuhimu wa zawadi ya maisha na Injili; upendo na huruma ya Mungu na wala si fedha wala uchu wa madaraka. Hata mtu akijitaabisha kiasi gani hawezi kuongeza hata siku moja ya maisha yake.

Baba Mtakatifu anawashukuru viongozi, wanafunzi na wadau waliotoka sehemu mbali mbali za Italia ili kuhudhuria tukio hili la kihistoria na kwamba, anawapongeza kwa ajili ya majitoleo yao na kazi wanayoifanya Hospitalini hapo. Anawaambia kwamba, bado anaendelea kujipanga ili aweze kutekeleza nia ya kukutana na kuzungumza nao mapema iwezekanavyo. Jambo la msingi ambalo linapaswa kukumbukwa ni kwamba, binadamu si mmiliki wa maisha yake na hawezi kuyatumia kadiri anavyotaka. Watu wakubali udhaifu wa mwili na kuendelea kumtumainia Mungu kwamba, ndiye nguvu yao!







All the contents on this site are copyrighted ©.