2014-07-14 11:42:22

Mahojiano na wasio amini yanalenga kuwaonjesha huruma na upendo wa Mungu!


Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anasema, Bwana Eugenio Scalfari mmiliki wa Gazeti la "La Republica" linalochapishwa kila siku nchini Italia hivi karibuni alifanya mahojiano maalum na Baba Mtakatifu Francisko kuhusu nyanyaso za kijinsia dhidi ya watoto wadogo, Kanisa pamoja na Mafia, mambo ambayo yanavuta na kugusa hisia za wasomaji wengi kwa nyakati hizi. Lakini kuna baadhi ya maneno ambayo yametumiwa na mwandishi huyu ambayo kimsingi hayaoneshi uhalisia kwamba, yametamkwa na Baba Mtakatifu Francisko, bali mawazo ya mwandishi mwenyewe!

Mahusiano kati ya Papa Francisko na waamini; maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, Yesu wa Nazareti pamoja na Mapokeo ya Kanisa ni kati ya mambo ambayo Baba Mtakatifu Francisko amejaribu kuyajibu katika mahojiano maalum na Bwana Scalfari. Anapenda kufanya mahojiano na watu wasioamini ili kuwamegea upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya watoto wadogo ni jambo la kusikitisha sana, kwani linawadumaza watoto katika makuzi na malezi yao, kiasi cha kushindwa kujenga na kuimarisha utu wao.

Watoto na vijana wanapaswa kupewa elimu makini katika maisha yao. Nyanyaso za kijinsia ni matendo ya udhalimu yanayoambatana pamoja na matumizi haramu ya dawa za kulevya. Kanisa litaendelea kutoa mchango wake kwa kukazia umuhimu wa elimu na majiundo makini ya binadamu. Kanisa halitawavumilia wale wanaojihusisha na nyanyaso kwa watoto wadogo. Yesu alionesha huruma na mapendo kwa wadhambi, lakini alikemea kwa ukali Pepo wabaya. Watu watubu na kumwongokea Mungu, ili kuachana na tabia ambayo ni kinyume kabisa cha ubinadamu na utu wema. Waamini wajenge na kudumisha dhamiri nyofu.

Baba Mtakatifu anakiri wazi kwamba, hafahamu kwa undani sana dhana ya "Mafia" lakini anatambua madhara yanayosababishwa na Mafia. Anaendelea kujisomea na kusikiliza shuhuda zinazotolewa na watu mbali mbali. Mafia ni kama ugonjwa ambao watu wanaambukizana, kiasi kwamba, dhamiri inakufa na kwao hawaoni tena sababu ya kuungama dhambi zao ili kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani. Watu wanaojihusisha na vitendo vya mafia wanasaidiana na kufichiana siri. Kanisa litaendelea kupambana na mafia kwani imejichimbia katika maisha na vipaumbele vya watu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema anaendeleza changamoto za majadiliano ya kidini na kiekumene yaliyoanzishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Majadiliano ya kiekumene yanakabiliwa na changamoto zake hasa kuhusiana na suala zima la useja! Viongozi wa Makanisa mengine wanaoa, lakini kwa Kanisa Katoliki, useja ni sehemu ya sifa na sadaka inayopaswa kutolewa na Makleri. Useja kwa Kanisa Katoliki ulianzishwa kunako Karne ya tano baada ya Kristo, ni zawadi inayokabiliwa na changamoto nyingi!







All the contents on this site are copyrighted ©.