2014-07-14 09:53:29

Hata wewe pia ni mpanzi! Je, umepanda nini?


Baba Mtakatifu Francisko katika tafakari yake wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 13 Julai 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican anasema kwamba, Yesu katika mahubiri yake, alitumia mifano na lugha iliyokuwa inaeleweka kwa watu wa nyakati zake. Mfano wa mpanzi unafafanuliwa na Yesu mwenyewe kwa kuelezea jinsi ambavyo mbegu iliyoanguka katika udongo inavyoweza kunyauka au kuzaa matunda yanayokusudiwa.

Yesu aliwafafanulia pia wafuasi wake maana ya mifano aliyokuwa anatumia katika mahubiri yake. Anasema mbegu iliyopandwa karibu na njia inaonesha wale wanaosikia Neno la Mungu lakini wanashindwa kulipokea, hivyo mwovu anapokuja hulinyakua Neno hili lililopandwa mioyoni mwao. Ile mbegu iliyoangukia penye miamba ni watu wanaolisikia Neno la Mungu na kulipokea kwa furaha, lakini Neno hili halina mizizi katika maisha ya watu hawa, panapotokea shida na mahangaiko, wanapoteza dira na mwelekeo.

Neno lililopandwa penye miiba, ni watu wanaosikiliza Neno la Mungu lakini kutokana na kumezwa mno na malimwengu pamoja na tamaa ya mali wanashindwa kuzaa matunda yanayokusudiwa. Mwishoni, mbegu iliyopandwa penye udongo mzuri ni wale watu wanaosikia Neno la Mungu, wakalipokea, wakalitunza na kulielewa, kiasi cha kuzaa matunda ajaa. Bikira Maria ni kielelezo makini cha udongo mzuri.

Baba Mtakatifu anawakumbusha waamini kwamba, wao ni udongo ambao Yesu mwenyewe anaendelea kupandikiza Neno na Upendo wake, hapa changamoto kwa kila mwamini ni kujiuliza, Je, hali yake ya moyo iko namna gani kadiri ya mifano iliyotolewa na Yesu. Waamini watambue kwamba, hata wao pia ni wapanzi, wanaopaswa kujichunguza kutoka katika undani wao, ili kutambua ni mbegu gani ambayo inatoka mioyoni na midomoni mwao, ili kuipandikiza!

Maneno yanaweza kuponya au kuangamiza; yanaweza kuwatia watu moyo au kuwakatisha tamaa, kumbe jambo la msingi ni kutambua hapa si kile kinachomwingia mtu, bali hasa kile kinachotoka moyoni mwa mtu. Bikira Maria awe ni mfano wa wale wanaolipokea Neno la Mungu na kuzaa matunda yanayokusudiwa!







All the contents on this site are copyrighted ©.