Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 15 ya Kipindi cha Mwaka wa A Kanisa
Wapendwa taifa la kikuhani, karibuni katika tafakari yetu Dominika ya 15 ya mwaka
A wa Kanisa. Leo Nabii Isaya, Mtakatifu Paulo na Mwinjili Matayo wanatuambia kuwa
Neno la Mungu likishaletwa kwetu haliachi kuzaa matunda hata kama kuna vipingamizi.
Kumbe wajibu wetu ni kuvumilia na kuendelea kuliishi mpaka tufikie ukamilifu katikai
maisha ya uzima wa milele.
Neno la Mungu
ni ufunuo wa Mungu, kumbe si jambo la leo na kesho bali ni uzima uliofunuliwa kwetu.
Neno hili lililo sauti ya Mungu kwetu halibadiliki kwa sababu ya kukutana na mazingira
magumu au mepesi, bali huendelea kutimiza kazi yake ya ukombozi. Sisi tuliolipokea
tuna wajibu wa kuvumilia magumu na mateso ili tuweze kurithi matunda yake.
Nabii
Isaya anaagua neno hili la Mungu wakati Waisraeli wako utumwani. Wana mashaka na wanamlalamikia
Mungu maana muda unapita na Mungu hatekelezi ahadi yake. Hatimaye Mungu anaibua kati
yao, nabii Isaya awatie moyo akiwakumbusha kuwa ahadi za Mungu ni za milele, hazibadiliki.
Anawafundisha kwa kutumia mfano wa mvua inyeshayo kuwa mara inyeshapo hairudi angani
bali hurutubisha ardhi ili iweze kuzaa matunda. Kumbe ahadi ya Mungu ya kuwatoa katika
utumwa wa kiroho na kimwili haitasimama kamwe na wala haibadiliki. Ndiyo kusema, neno
la Mungu tulilolipokea halitarudi bure bali litazaa matunda.
Kutokana na fundisho
hili tunaitwa kukumbuka kuwa kazi ya Mungu inayotendwa kwa njia yetu na hasa kazi
za upendo zaweza kuwa na vipingamizi vingi lakini tusiogope. Bwana yu pamoja nasi.
Tutoe mfano mmojawapo: jamaa mmoja aliwahi kuniambia hapendi kufunga ndoa kwa sababu
baadhi ya waliofunga ndoa wameachana yaani wametengana! Nikasema: neema na makusudio
ya Mungu hayaondolewi na shida kama hiyo kwa maana nia ya Mungu ni ya milele. Ataendelea
kuwasaidia wale wote wanaojinyenyekeza na kuomba neema zake kila siku. Kumbe ndoa
yadai maisha ya sala yaunganishayo mnyororo wa neema za Mungu. Kama kweli Mungu anakuita
kwa wito huo atakupa neema kukuwezesha kuutimiza vema.
Mfano wa mpanzi katika
injili unaoelezwa kwa picha ya mbegu zinazoanguka katika mwamba, njiani, katikati
ya miiba na penye udongo tifutifu ni kielelezo cha vipingamizi katika kupokea imani
na kuiishi. Ni picha ya ugumu na wepesi uliopo katika kueneza Neno la Mungu. Hata
hivyo mwinjili anatutia moyo akisema kwa vyovyote vile injili ya Kristu itazaa matunda.
Natumai ndugu waamini mmewahi kujikuta katika mazingira ya ugumu katika kuishi imani
yenu, je mlikata tamaa? Hapana mlisonga mbele!
Mtakatifu Paulo anasema mateso
na magumu ya leo si kitu ukilinganisha na faida tutakayopata tutakapomwona Mungu uso
kwa uso ndiyo kurithi nchi aliyoahidiwa babu yetu Ibrahimu! Zaidi ya hilo anasema,
je, njaa yaweza kututenga na upendo wa Kristu? Hapana, Kumbe tunaalikwa kuvumilia
mateso na magumu mpaka mwisho mambo yatakapokamilika katika Kristu Yesu Mkombozi.
Niwatakie
siku njema ya Bwana nikiwaomba kuimarika zaidi na zaidi mnapokutana na ugumu katika
kutangaza injili ya Kristu katika maisha yenu. Tumsifu Yesu Kristo Tafakari hii
imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya cpps