Athari za myumbo wa uchumi kimataifa, vita, kinzani na migogoro bila kusahau magonjwa
na majanga mbali mbali yanayoendelea kumwandama mwanadamu katika maisha yake. Yote
haya ni mambo yanayochangia kwa watu wengi kukata tamaa ya maisha na hivyo kujiona
kuwa si mali kitu na kwamba, kwao maisha hayana tena dira wala mwelekeo!
Katika
mazingira kama haya, watu wanapata "kigugumizi" cha kufanya maamuzi magumu katika
maisha yao: kwa mfano vijana kufunga ndoa na kuanza maisha ya unyumba kwa kutambua
kwamba, ndoa kati ya Bwana na Bibi kadiri ya Mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu
ni zawadi ya kudumu! hali kama hii inaweza kuwakuta hata vijana wanaotaka kujiunga
na maisha na wito wa Kipadre na Kitawa!
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe
wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii anawahamiza waamini na watu wote wenye mapenzi
mema kujiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu: wawe tayari kutekeleza wito na mwaliko
wake, kwani kwa lolote analowataka kulifanya atawakirimia maradufu!