2014-07-10 08:49:44

Jengeni utamaduni wa amani!


Baraza kuu la Shirikisho la Wanahabari Wakatoliki, SIGNIS katika mkutano wake uliofanyika hivi karibuni huko Bruselles umeamua kwamba, katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia sasa, SIGNIS itajielekeza zaidi katika mchakato wa kuvisaidia vyombo vya habari kujikita katika ujenzi wa utamaduni wa amani. SIGNIS inapenda kushiriki katika ujenzi wa utamaduni wa amani sehemu mbali mbali duniani kwa kuwapatia watu habari za matumaini mintarafu utamaduni wa dijitali. RealAudioMP3

Baraza linataka kujielekeza zaidi katika kupambanua mikakati ya mawasiliano ili kufanya maboresho makubwa katika matumizi ya mitandao ya kijamii. Hiki ni kikao cha kwanza kufanywa na Baraza hili chini ya Bwana Gustavo Andùjar pamoja na makamu wake wawili.

Itakumbukwa kwamba, katika maadhimisho ya mkutano mkuu wa SIGNIS Kimataifa uliofanyika mjini Roma, Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, katibu mkuu wa Vatican, aliwahimiza wajumbe kufanya tafakari ya kina kuhusu nguvu ya mawasiliano ya jamii kwa njia ya picha zinazotumiwa na vyombo vya mawasiliano ya jamii, ili kuonesha na kuwajengea watazamaji matumaini na kuwaondolea mashaka vijana wa kizazi kipya.

Ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, unaonekana kuwa na utamaduni, lugha na alama mpya kiasi cha kutengeneza taswira ya jumla. Baba Mtakatifu Francisko aliwataka Wanahabari Wakatoliki kukabiliana na changamoto za njia za mawasiliano ya kijamii, ili kuwashirikisha watu: hekima, ukweli na uzuri wa Injili, katika lugha ambayo inaleta mguso na mashiko katika: akili na mioyo ya watu, kwani kuna watu wengi wanaotafuta maana ya maisha yao.








All the contents on this site are copyrighted ©.