2014-07-09 10:19:08

Usalama barabarani!


Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao! Ndiyo kauli mbiu iliyoongoza Siku ya Usalama Barabarani Kitaifa nchini Hispania, iliyoadhimishwa Jumapili iliyopita, tarehe 6 Julai 2014 kwa kuwataka waamini na wananchi wa Hispania kuwa makini katika matumizi ya barabara pamoja na kutoa kipaumbele cha pekee kwa watu wanaokutana nao kila siku ya maisha yao wanapokuwa barabarani!

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania katika ujumbe wake kwa maadhimisho ya Siku hii wanasema kwamba, kuna haja ya kuwa na mwelekeo chanya unaojikita katika: upendo, ukarimu, majadiliano, hali ya kusikilizana na kuheshimiana pamoja na kusaidiana pale inapowezekana badala ya kuwa na mwelekeo potofu, unaoonesha jeuri, kiburi na malumbano yasiyo na tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya mtu: kiroho na kimwili.

Maaskofu wanawahamasisha waamini na wananchi katika ujumla wao kuonesha upendo na mshikamano na watu wanaokutana nao katika hija ya maisha yao ya kila siku, kwani kila mtu anaweza kuwa kweli ni msaada kwa jirani yake kama ilivyotokea kwa Wafuasi wa Emmau walipokutana na kuanza kuandamana na Yesu, hatimaye, wakamtambua katika kuumega Mkate! Tangu wakati ule wakabadilika na kuwa watu wapya zaidi!

Maaskofu Katoliki Hispania wanawaalika waamini kutoa nafasi kwa Yesu ili aweze kuandamana nao katika hija ya maisha yao, kwani Yesu ni Bwana, Mwalimu na Rafiki. Ikiwa kama kweli waamini na wananchi wa Hispania watamwachia Yesu nafasi katika maisha yao ili aweze kuwaongoza hata ajali barabarani zinaweza kupungua kwa kuwajali zaidi watumiaji wote wa barabara.

Maaskofu kwa kushirikiana na Serikali ya Hispania wamekuwa wakiendesha kampeni ya usalama barabarani kiasi kwamba idadi ya vifo vinavyotokana na ajali barabarani vimepungua na kufikia watu 1, 128 katika kipindi cha mwaka 2013. Hiki ni kiwango kidogo kabisa cha vifo vinavyotokana na ajali barabarani tangu mwaka 1960. Watu wakiamua kufuata sheria na kanuni za usalama barabarani kuna uwezekano kabisa wa kuokoa maisha ya watu.

Watumiaji wa barabara wanakumbushwa kwamba, maisha ya binadamu ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu wasiridhike na mafanikio haya, bali walenge zaidi kujieousha na ajali barabarani. Watumiaji wa barabara wawe makini na wawajibike kwa maisha yao binafsi na yale ya watumiaji wengine wa barabara!







All the contents on this site are copyrighted ©.