2014-07-09 09:53:08

Kimeeleweka!


Askofu Evaristo Changula wa Jimbo Katoliki Mbeya, hivi karibuni ametabaruku Kanisa na kuzindua Parokia Mpya ya Mtakatifu Yohane Paulo II, iliyoko eneo la Ilomba, Jimbo Katoliki la Mbeya kwa kuitaka Familia ya Mungu Jimboni humo kuchuchumilia utakatifu na ushuhuda wa maisha adili. Pale wanapojikuta wameelemewa na dhambi pamoja na mapungufu yao ya kibinadamu, wakimbilie huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Sakramenti za Kanisa.

Askofu Chengula amewataka waamini kuwasaidia na kuwaombea Mapadre wao, ili waweze kutekeleza vyema huduma ya Neno la Mungu, maadhimisho ya Mafumbo ya Kanisa pamoja na huduma ya upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Anawataka pia wanafamilia kuwa kweli ni mfano wa kuigwa ndani ya Jamii kwa kujikita katika maisha adili na matakatifu, huku wakisaidiana kumpeleka Kristo katika Familia zao ambazo kimsingi ni Kanisa dogo la nyumbani, shule ya sala na utakatifu wa maisha.

Waamini wa Parokia Mpya ya Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili Jimbo Katoliki Mbeya wanabahati sana kuwa na Msimamizi ambaye alisimama kidete kulinda na kutetea Injili ya uhai, maisha na utakatifu wa ndoa na familia; ni Mtakatifu aliyekazia umuhimu wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili na kwamba, ni Mtakatifu aliyetamani kuona haki na amani vikitawala katika maisha ya watu sehemu mbali mbali duniani. Hii ndiyo changamoto kubwa inayopaswa kufanyiwa kazi na Waamini wa Parokia Mpya ya Mtakatifu Yohane Paulo II.

Ujenzi wa Parokia hii ulikuwa unaongozwa na kauli mbiu ni "Hadi kieleweke" na kwa hakika sasa kimeeleweka na Familia ya Mungu imepta Parokia ambayo lengo lake kuu ni kusogeza huduma za kichungaji kwa waamini. Mafanikio ya ujenzi wa Kanisa hili tangu hatua za awali kabisa ni kielelezo cha ukarimu kilichooneshwa na wazee waliotoa kiwanja kunako miaka 1970 kwa ajili ya ujenzi wa Kigango ambacho leo hii ni Parokia.

Kabla ya ujenzi wa Kigango, waamini walikuwa wanasali darasani, baadaye wakapata chumba kilichokuwa na matumizi mchanganyiko, Jumapili asubuhi Ibada ya Misa Takatifu, jioni wazee walikuwa wanajirusha kwa kujipongeza kwa kinywaji baridi. Parokia ya Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili imefika kwa wakati muafaka kabisa wanasema waamini kwani wakati huu kuna mwamko mkubwa sana wa kutaka kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Kwa hakika kimeeleweka!

Na Thompson Mpanji,
Mbeya, Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.