2014-07-09 12:30:40

Jifungeni kibwebwe kwani mambo baado kabisa!


Kanisa Katoliki nchini Malawi linamshukuru Mungu kwa maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Malawi pamoja na mafanikio makubwa yaliyokwishapatikana katika kipindi chote hiki kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Malawi. Lakini bado Malawi inapaswa kujifunga kibwebwe kuhakikisha kwamba, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa vinalindwa na kuendelezwa kwa kutambua kwamba, amani ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomwajibisha binadamu!

Bado Malawi haina budi kujielekeza katika maboresho ya huduma ya afya na elimu kwa wananchi wake. Uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Malawi hivi karibuni na kumpatia ushindi Professa Arthur Peter Mutharika kuwa Rais wa Malawi ni nafasi ya kufanya tafakari ya kina kuhusu demokrasia na ukomavu wa kisiasa nchini Malawi sanjari na ujenzi wa misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa.

Ni changamoto ambayo imetolewa na Padre George Buleya, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi katika kilele cha maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Uhuru wa Malawi, iliyofanyika hapo tarehe 6 Julai 2014. Kanisa limetumia fursa hii kwa ajili ya kusali na kuiombea Malawi na wananchi wake, ili waendelee kushikamana kwa pamoja, ili kujiletea maendeleo endelevu yanayozingatia ustawi wa mtu mzima: kiroho na kimwili.

Padre Buleya anasema, kimsingi wananchi wa Malawi ni watu wanaopenda amani na maendeleo. Miaka hamsini iliyopita kulikuwa na ari pamoja na moyo wa uzalendo nchini Malawi, lakini tunu hizi msingi zinaendelea kutoweka siku hadi siku. Kuna haja ya kuendelea kuwekeza katika maboresho ya huduma msingi za elimu, afya na maendeleo endelevu, uhakika na usalama wa chakula kwa wananchi wote wa Malawi, kama ambavyo pia amekazia Rais Mutharika katika hotuba yake.

Malawi inapaswa pia kukabiliana na tatizo la rushwa na ufisadi wa mali ya umma mambo ambayo katika miaka ya hivi karibuni yameitumbukiza Serikali ya Malawi katika kashfa kubwa kiasi kwamba, baadhi ya Nchi wahisani ziliamua kusitisha misaada yake katika bajeti ya Malawi, hali ambayo imefifisha utoaji wa huduma msingi kwa wananchi wa Malawi.







All the contents on this site are copyrighted ©.