Umoja wa Mataifa unaonya kwamba, mashambulizi ya mara kwa mara yanayofanywa na vikosi
vya Al Shabaab pamoja na kinzani za kijamii, kisiasa na kiuchumi nchini Somalia zinaweza
kuitumbukiza tena Somali katika baa la njaa. Ukame bado umetanda kutokana na mvua
kidogo iliyonyeesha mwaka huu. Yote haya yanachangia uwezekano wa baa la njaa kuzuka
tena nchini Somalia, ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa haitachukua hatua za dharura
kukabiliana na hali hii.
Uhaba wa chakula nchini Somalia unachangiwa pia na
mfumuko wa bei ya mazao ya chakula, hali ambayo inaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa
tatizo la utapiamlo wa kutisha miongoni mwa watoto wadogo wenye umri chini ya miaka
mitano. Umoja wa Mataifa unakaidiria kwamba, watu zaidi ya 250, 000 wamefariki dunia
nchini Somalia kutokana na baa la njaa na kwamba, zaidi ya watoto 200, 000 wanakabiliwa
na utapiamlo mkali.
Ukosefu wa chakula nchini Somalia umeendelea kukua na
kuongezeka na kwa sasa Umoja wa Mataifa unasema hali ni mbaya, kiasi kwamba, kunahitajika
kupanga mikakati ya dharura kwa watu ambao wako hatarini kufa kwa baa la njaa nchini
Somalia!