2014-07-08 10:58:41

Vyombo vya habari saidieni mchakato wa amani na utulivu


Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya katika ujumbe wake kwa vyombo vya habari wakati huu ambapo Kenya inaendelea kukabiliana na mashambulizi ya kigaidi kiasi cha kutishia amani na usalama wa wananchi, linavitaka vyombo vya habari nchini humo, kusaidia mchakato wa ujenzi wa upatanisho, haki, amani na utulivu kati ya watu!

Maaskofu wanawataka wananchi wote wa Kenya kuondokana na masuala yote yanayoweza kuwagawa na hivyo kudhohofisha umoja wa kitaifa kwa kujikita katika misingi ya ukabila na siasa. Kwa sasa Kenya inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa ulinzi na usalama, kinzani na misigano ya kisiasa, ukabila, rushwa na ufisadi.

Haya ni mambo ambayo yanatishia amani, usalama, umoja na mshikamano wa kitaifa. Wanasiasa katika ngazi mbali mbali wanapaswa kujielekeza zaidi katika ujenzi wa mambo msingi yanayowaunganisha wananchi wote wa Kenya, kwa kujikita katika utawala bora unaozingatia kanuni na sheria za nchi. Ujumbe wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya umetiwa sahihi na Padre Vincent Wambugu, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya.

Hivi karibuni, Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya lilikutana na kuzungumza na Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya kuhusu hali tete inayoendelea kujitokeza nchini Kenya kwa sasa. Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linavitaka vyombo vya habari kusaidia mchakato wa ujenzi wa misingi ya amani na utulivu badala ya kushabikia maandamano na kinzani za kisiasa.







All the contents on this site are copyrighted ©.