2014-07-08 09:07:17

Bado tunakumbuka!


Wakimbizi na wahamiaji wengi wanaendelea kuteseka kiasi kwamba, utu na heshima yao kama binadamu vimewekwa rehani. Hawa ni wahanga wa utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko pamoja na mateso ya watu wengine. RealAudioMP3

Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuonesha mshikamano wa upendo kwa wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta usalama na ubora wa maisha ughaibuni kwa kukimbia: vita, nyanyaso, madhulumu, kinzani za kijamii, kisiasa, kidini na kikabila.

Ni watu ambao wameelemewa na kongwa la umaskini pamoja na majanga asilia, kiasi kwamba, hawana tena matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi. Tarehe 8 Julai 2013, Baba Mtakatifu Francisko alitembelea Kisiwa cha Lampedusa, kilicho kusini mwa Italia, ili kuonesha mshikamano wa upendo na wahamiaji pamoja na wakimbizi wanohatarisha maisha yao wakiwa njia kutafuta nafuu na ubora wa maisha.

Kardinali Antonio Maria VegliĆ², Rais wa Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalu, Jumapili iliyopita ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumbu kumbu ya mwaka mmoja tangu Baba Mtakatifu Francisko alipotembelea Kisiwa cha Lampedusa.

Tangu wakati huo, bado kuna maelfu ya watu wanaoendelea kupoteza maisha yao kwa kufa maji na utupu Jangwani. Kumbu kumbu hii anasema Kardinali Veglio ni kutaka kuamsha tena dhamiri ya Jumuiya ya Kimataifa ili iweze kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya wahamiaji na wakimbizi wanaokufa maji baharini. Watu wajiulize ni jambo gani ambalo limewagusa tangu walipoona majeneza ya wahamiaji na wakimbizi yamejipanga Kisiwani pale!

Ili kujenga na kuimarisha utamaduni wa upendo na mshikamano kuna haja ya kuwa na mtazamo mpya kuhusu wahamiaji na wakimbizi, kwa kujenga na kuimarisha utamaduni wa watu kukutana ili kuonjeshana ukarimu kwa kumwangalia mkimbizi na mhamiaji kama binadamu anayepaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa, licha ya matatizo na changamoto anazokumbana nazo!

Hawa ni watu wanaohatarisha maisha yao kiasi cha kutembea na kifo machoni pao. Hawa ni watu wanaotoka katika nchi zile ambazo kuna vita, dhuluma na nyanyaso za utu na heshima ya binadamu.

Katika kipindi cha miezi kadhaa iliyopita, watu zaidi 75, 000 wametua nanga ya matumaini Kusini mwa Italia. Kufunga mipaka kwa watu kama hawa si suluhisho ya kudumu, kwani ni kundi ambalo linaweza kuangukia katika mikono ya wafanyabiashara ya binadamu! Upendo na mshikamano ni jambo la kupewa kipaumbele cha kwanza!








All the contents on this site are copyrighted ©.