2014-07-07 11:54:33

TEC yawaomba wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kuachana na ubinafsi


Kwa mujibu wa Gazeti la” This Day” Askofu Tarcius Ngalelakumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania(TEC) akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki, alisema, TEC imefadhaishwa na kuzuka kwa mabishano makali na mpasuko uliosababisha upotoshaji wa nia iliyo kusudiwa ya kuunda Bunge Maalum la Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.

Askofu Ngalelakumtwa, alitumia nafasi hiyo kukumbusha kwamba, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Jakaya Kikwete, kwa ujasiri wa kipekee alianzisha mchakato wa kuunda katiba mpya, na kisha aliridhia kwa furaha , kuipokea rasimu ya pili ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Lakini kutokana na hali ya mvutano mkali na utengano uliojitokeza katika Bunge maalum la Katiba, Rais wa TEC, ametoa wito kwa Watanzania, kujiuliza nini kimetokea hadi mwelekeo mzima wa mabadiliko ya Katiba kugeuka kabisa kwa kuikejeli na kuishutumu vikali rasimu hiyo, ambayo inatakiwa kuandika historia ya kipekee ya Bunge Maalum la Katiba. pia inashangaza jinsi wajumbe wake walivyo sahau gharama kubwa, iliyo bebeshwa walipa kodi wakati wakiiijadili, na sasa majadiliano hayo yanaonyesha dhahiri kutaka kuiingiza nchi katika mgogoro mkubwa unaoashiria hatari mbele.

Rais wa TEC anaendelea kusema, wakati wa uzinduzi, Rais Kikwete aliweka wazi msimamo wake kwamba rasimu ya pili ya Katiba ilikuwa na kasoro nyingi na kusema kwamba wajumbe wa Bunge hilo wanapaswa kusoma ukurasa kwa ukurasa, sentensi kwa sentensi, neno kwa neno na wakiona kuna mambo ya kubadilisha wayabadilishe.

Kumbe tatizo liko wapi? Askofu Tarcisio Ngalelakumtwa, ametaja maoni ya TEC katika mgogoro huu wa Katiba kwamba, ni kukosekana kwa utashi na uwajibikaji wa kisiasa na wajumbe kutokuwa wakweli juu ya suala zima la mchakato wa Katiba. TEC imewataka wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kuwa wamoja na kufanya kazi yao kwa mtazamo usioegemea siasa za vyama, ili mchakato uwezeshe upatikanaji wa katiba mpya.“Kuandika katiba ni kazi iliyo ngazi ya juu zaidi ya siasa za vyama, hivyo utashi wa kisiasa wa kuunda Katiba mpya kwa kuzingatia rasimu ya pili utaweza kuridhiwa kwa kuzingatia msingi huu,” alisema Rais huyo ambaye pia ni Askofu wa Jimbo la Iringa.

Na aliwaasa kwamba , “iwapo matokeo yatakuwa yenye kuleta mema na kuimarisha amani na utulivu Tanzania, watu wote watawashukuru na kuwasifu, lakini kama tunda la kazi yao litakuwa la kuingiza nchi kwenye matatizo zaidi, ni kuwataabisha wananchi na kukosa maelewano baina yao, basi watu watawahukumu na kuwawajibisha kwa kukosa umakini katika jukumu walilokabidhiwa”









All the contents on this site are copyrighted ©.