Baraza la Maaskofu Katoliki DRC, CENCO, limemsihi Rais Joseph Kabila wa DRC kuheshimu
Katiba ya nchi ambayo kimsingi ni sheria mama na kuachana kabisa na wazo la kutaka
kubadili Katiba, ili kupata nafasi ya kuweza kushiriki tena katika kinyang'anyiro
cha urais wakati wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini humo kunako mwaka
2016.
Kutaka kung'ang'ania madarakani, kunaweza kutibua mustakabali na maendeleo
ya DRC ambayo hadi sasa inaendelea kuchechemea kutokana na vita na kinzani za kijamii
na kisiasa. Uchu wa mali na madaraka umepelekea wananchi wengi Barani Afrika kujikuta
wanakabiliana na majanga mbali mbali ya maisha, mambo ambayo yamekwamisha mchakato
wa kujiletea maendeleo endelevu hata kama nchi hizi zina utajiri na rasilimali ya
kutosha ambayo ingesaidia kupambana na baa la umaskini, njaa na maradhi.
Baraza
la Maaskofu Katoliki DRC katika ujumbe wake kwa maadhimisho ya Uhuru wa DRC, hivi
karibuni, linaonya kwamba, wazo la kutaka kupindisha katiba linaweza kuvuruga umoja
na mshikamano wa kitaifa, changamoto ambayo imetolewa pia na wawakilishi wa Jumuiya
mbali mbali za Kimataifa nchini DRC. Rais Joseph Kabila alishinda kwenye uchaguzi
uliofanyika mwaka 2006 na kupata tena ridhaa ya wananchi ya kuwaongoza kunako mwaka
2011 na sasa anataka kubadili Katiba ili aweze kushiriki tena katika uchaguzi wa Mwaka
2016.
Baraza la Maaskofu Katoliki DRC linaitaka Serikali kuanza mchakato wa
zoezi la kupiga kura mapema, kama sehemu ya kuwajengea wananchi uwezo wa kushiriki
katika demokrasia, ustawi na maendeleo yao.