2014-07-06 08:24:34

Baba Mtakatifu bado anawalilia wahamiaji wanaokufa maji wakiwa njiani kwenda Ulaya!


Askofu mkuu Francesco Montenegro wa Jimbo kuu la Agrigento, Kusini mwa Italia, Jumamosi jioni tarehe 5 Julai 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumbu kumbu ya mwaka mmoja tangu Baba Mtakatifu Francisko alipotembelea Kisiwa cha Lampedusa kushuhuhudia mwenyewe kwa macho yake mateso na mahangaiko ya wahamiaji waliokuwa wanakufa maji na kiu jangwani wakati wakiwa njiani kuelekea Barani Ulaya.

Itakumbukwa kwamba, hija hii ilifanywa na Baba Mtakatifu hapo tarehe 8 Julai 2013. Tangu wakati huo kuna wahamiaji wengi wameendelea kufa maji baharini.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa ajili ya kumbu kumbu hii, anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumwezesha kutembelea Lampedusa, ili kuonesha mshikamano wake na wahamiaji pamoja na kusali kwa ajili ya kuwaombea maelfu ya watu wanaokufa maji baharini, wakiwa njiani kutafuta unafuu wa maisha pamoja na kuamsha dhamiri za watu ili waweze kuguswa na mateso ya watu hawa.

Baba Mtakatifu anawashukuru na kuwapongeza wananchi wa Lampedusa kwa upendo na mshikamano wanaouonesha kwa wahamiaji. Shukrani hizi zinawaendea pia wananchi wote wa Italia ambao kweli wameonesha moyo wa upendo na mshikamano kwa wahamiaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Ni vigumu kupokea misiba ya wahamiaji wanaokimbia majanga ya maisha; umaskini, vita na kinzani ambazo wakati mwingine zinauhusiano wa moja kwa moja na siasa za kimataifa.

Baba Mtakatifu anasema wakati huu anapenda kuungana nao kiroho ili kuwalilia wahamiaji wanaoendelea kufa maji baharini pamoja na wote wanaotupa mashada ya maua ya sala kwa ajili ya kuwakumbuka wahamiaji hawa, wanaopaswa kushughulikiwa kikamilifu badala ya kuwageuzia kisogo, bali kwa kuwaonjesha upendo na ukarimu, kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu, heshima na haki zao msingi, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu na wala si vinginevyo!

Baba Mtakatifu anaendelea kuzihimiza Jumuiya za Kikristo pamoja na watu wenye mapenzi mema kuendelea kuwaonjesha upendo na mshikamano wale wote wanaohitaji bado msaada wao, bila kudai, kuogopa, bali kwa kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko yao. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, taasisi za kimataifa zitajitahidi kuonesha ujasiri na ukarimu kwa wakimbizi na wahamiaji, ili kupata ufumbuzi wa kudumu katika matukio haya!







All the contents on this site are copyrighted ©.