2014-07-05 14:02:06

Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa kuongoza tena kwa kipindi cha miaka mitano!


Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni amethibitishwa tena kuendelea na utume wake katika kipindi cha miaka mitano tena kuanzia sasa. Huu ni uamuzi uliofanywa na Kamati kuu ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni iliyokuwa inafanya kikao chake mjini Geneva hapo tarehe 3 Julai 2014. Dr Tveit amepokea dhamana hii kwa mara nyingine tena kwa moyo mkuu na shukrani.

Miaka mitano iliyopita, imekuwa ni miaka ya neema na baraka tele kwa Baraza la Makanisa Ulimwenguni na sasa Baraza litaendeleza hija yake ya maisha ya kiekumene, ili kukabiliana na matatizo, changamoto na mapungufu mbali mbali yanayoendelea kujitokeza katika maisha na utume wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni. Hii ni nafasi nyingine tena inayomwimarisha katika maisha na utume wake kama Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anasema Dr. Tveit.

Taarifa inaonesha kwamba, miaka kadhaa iliyopita, Dr. Tveit amejitahidi kuimarisha mahusiano kati ya Makanisa duniani pamoja na kuendelea kuhamasisha Jumuiya za Kikristo kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki na amani. Ni matumaini ya Dr. Tveit kwamba, ataendeleza kazi na utume wake aliouanza kwenye awamu yake ya kwanza ya uongozi wake kama katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, ili kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Makanisa Ulimwenguni.







All the contents on this site are copyrighted ©.