2014-07-05 13:41:46

Kanisa linatumikia na kuishi katika uhuru ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu


Baba Mtakatifu Francisko baada ya kuzungumza na ulimwengu wa wafanyakazi, wakulima na wanafunzi, alikwenda moja kwa moja hadi kwenye Uwanja wa Michezo wa Campobasso ambako ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu iliyohudhuriwa na umati mkubwa wa waamini kutoka ndani na nje ya Jimbo kuu la Campobasso-Boiano, Jumamosi tarehe 5 Julai 2014. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake mintarafu Liturujia ya Neno la Mungu amekazia mambo makuu mawili katika maisha na utume wa Kanisa; kwamba, ni Watu wanaomtumikia Mungu na wanaishi katika uhuru ambao ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu mwenyewe. Huduma ya Watu wa Mungu inajionesha kwa namna ya pekee katika maisha ya Sala, Utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu na kwa njia ya ushuhuda wa upendo na katika mambo haya, Bikira Maria ni kielelezo na mfano wa kuigwa.

Kanisa katika shule ya Bikira Maria linajifunza kila siku kuwa ni "Mtumishi wa Bwana" kwa kusoma alama za nyakati ili kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kutoa kipaumbel cha pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Huduma ya upendo ni changamoto kwa kila mwamini inayopaswa kumwilishwa kila siku ya maisha, katika familia, parokiani, sehemu za kazi na kwa majirani.

Huduma ya upendo ni kielelezo makini cha Uinjilishaji na hapa Kanisa limeendelea kuwa katika mstari wa mbele kwa kuonesha umama na udugu katika kushirikiana na wahitaji, ili kuwajengea matumaini zaidi. Baba Mtakatifu anawashukuru waamini wa Jimbo kuu la Campobasso-Boiano kwa huduma wanayoifanya kwa kushirikiana na Askofu wao mahalia, changamoto na mwaliko wa kuendeleza huduma hii ya upendo, kwa kujenga na kuimarisha utamaduni wa mshikamano, ili kuwahudumia watu wenye mahitaji ya kiroho na kimwili, lakini hasa kwa wasiokuwa na fursa za ajira, jambo ambalo kwa sasa ni janga la kimataifa linalohitaji mshikamano wa dhati.

Kazi ni changamoto kubwa inayowawajibisha viongozi wa Serikali, wafanyabiashara na watunga sera. Hapa utu na heshima ya binadamu vinapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika mikakati na utekelezaji wake mambo mengine hata kama ni halali yanafuata baadaye.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuishi katika uhuru wa kweli unaotolewa na Mwenyezi Mungu ili kushinda ubinafsi na miundo yake yote, ili kujisadaka kwa moyo wa furaha kama alivyofanya Bikira Maria, kwa kuona na kuguswa na mahitaji ya wenye shida na mahangaiko zaidi; uhuru unaotekelezwa kwa njia ya upendo na kumwilishwa katika maisha ya Jumuiya za Kikristo wakati zinapojisadaka kwa ajili ya huduma kwa jirani, ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano.

Baba Mtakatifu anasema, uhuru wa Mungu unawawezesha waamini kuondokana na hali ya kukosa imani, masikitiko, woga na utupu katika maisha ya ndani; upweke, majonzi na litania ya malalamiko yasiokuwa na msingi. Hata katika Jumuiya za Waamini kuna watu wanaotaka kujilinda zaidi kuliko kujisadaka kwa ajili ya wengine, lakini wakijiachilia mikononi mwa Yesu anaweza kuwaokoa. Hata katika mapungufu yao kibinadamu na dhambi wanazotenda, bado wanahamasishwa kuwa na furaha na ujasiri ili kushuhudia imani yao kwa kujenga na kuimarisha umoja na Mwenyezi Mungu, ili kukabiliana kwa ujasiri mkubwa magumu na vishawishi vya maisha.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha mahubiri yake katika Ibada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Michezo wa Campobasso kwa kuwaombea waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutembea katika uhuru wa kweli waliopewa na Mwenyezi Mungu. Bikira Maria aliwezeshe Kanisa kuwa kweli ni Mama na mkarimu kwa wote; waoneshe upendo na mshikamano kwa wagonjwa na vijana na kwamba, Bikira Maria, Mama wa uhuru awe ni kielelezo cha faraja na matumaini thabiti!

Naye Askofu mkuu Giancarlo Bregantini kwa niaba ya waamini wake, amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuangalia unyenyekevu wa wananchi wa Molise na kuamua kuwatembelea. Amemshukuru kwa ushuhuda wa mapendo anaoendelea kuwaonjesha Watu wa Mungu; Utamaduni wa mshikamano ili kukabiliana na changamoto za maisha, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii pamoja na kuishi katika uhuru wa wana wa Mungu kwa kuiga mfano wa Bikira Maria.

Ni changamoto hii inayopaswa kufanyiwa kazi kwa kuwaonesha upendo na ukarimu wageni na wahamiaji, kwa kujikita katika ukweli na haki. Anawashukuru waamini na watu wote wenye mapenzi mema waliojisadaka kwa ajili ya kufanikisha hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko Mkoani Molise, Kusini mwa Italia.







All the contents on this site are copyrighted ©.