2014-07-04 12:20:10

Umoja na mshikamano wa kitaifa Kenya!


Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya hivi karibuni limekutana na kuzungumza na Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya kuhusu hali tete inayoendelea kujitokeza nchini humo na hasa misigano ya kisiasa inayohatarisha usalama, umoja na mshikamano wa kitaifa. Maaskofu wanatawaka wanasiasa nchini Kenya kuweka pembeni tofauti zao za kisiasa na kuanza kushughulikia masuala msingi kwa ajili ya ustawi na mafao ya wananchi wa Kenya.

Maaskofu wanaitaka Serikali kuharakisha mageuzi katika vikosi vya ulinzi na usalama, kubainisha sera na mikakati ya kukuza na kuendeleza uchumi pamoja upatikanaji wa fursa za ajira kwa vijana, kwani vijana wengi kwa sasa wanatumiwa na wanasiasa kwa ajili ya mafao yao binafsi pamoja na kupambana na umaskini.

Rais Uhuru Kenyatta kwa upande wake anasema, yuko tayari kukutana na kuzungumza na Wananchi wa Kenya kadiri ya sheria na katiba ya nchi. Serikali ya Kenya inaendelea kuongeza rasilimali watu na fedha ili kuimarisha ulinzi na usalama kwa raia na mali zao. Utawala wa sheria utaendelea kuimarishwa nchini Kenya na watambue kwamba, sheria ni msumeno.

Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini Kenya kuungana pamoja kusali ili kuombea amani, usalama na ustawi wa wananchi wote wa Kenya.







All the contents on this site are copyrighted ©.