2014-07-04 09:48:27

Tunzeni mazingira!


Askofu mkuu Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya ambaye pia ni mwakilishi wa Vatican kwenye Makao makuu ya Shirika la mazingira na makazi ya watu la Umoja wa Mataifa, hivi karibuni ameshiriki katika mkutano wa mazingira uliokuwa unafanyika Jijini Nairobi, Kenya kwa kukemea ulaji wa kupindukia na kwamba, umefika wakati kwa watu kubadili tabia hii. Vatican itaendelea kuunga mkono juhudi za Jumuiya ya Kimataifa katika kulinda na kutunza mazingira.

Ustawi na maendeleo ya binadamu kwa siku za usoni unategemea kwa kiasi kikubwa, jinsi ambavyo mwanadamu anavyojitahidi kulinda na kutunza mazingira, kwa kuzingatia misingi ya haki na usawa kwani mazingira ni zawadi ya kazi ya uumbaji ambayo mwanadamu amekabidhiwa kuitunza na kuiendeleza. Mwanadamu katika historia yake amekuwa ni chanzo kikuu cha uharibifu wa mazingira, changamoto kwa sasa kuonesha unyenyekevu, kiasi na kuanza kujikita katika kulinda na kutunza mazingira.

Askofu mkuu Balvo amewapongeza wajumbe wa mkutano mkuu wa mazingira ambao kwa mara ya kwanza katika historia umefanyika Jijini Nairobi kwa ngazi ya kimataifa, ili kutafuta njia, mbinu na mikakati ya kulinda, kutunza na kuendeleza mazingira, kwani mazingira ni kazi ya uumbaji inayowawajibisha binadamu. Amempongeza pia Marehemu Professa Wangari Maathai, kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utunzaji bora wa mazingira nchini Kenya, changamoto ya kuendeleza kazi ya uumbaji.

Vatican inafuatilia kwa umakini mkubwa mikakati na malengo yaliyoainishwa na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa kwa kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuratibu ulaji wa kupindukia, ili kuwa na ustawi na maendeleo kwa siku za usoni, kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Ikumbukwe kwamba, rasilimali ya dunia ni kwa ajili ya mafao ya wote. Lakini, uzoefu unaonesha kwamba, kuna baadhi ya watu wenye uchu wa mali na fedha wanaoendelea kuharibu mazingira kwa ajili ya mafao yao binafsi. Jamii inapaswa kujirekebisha kwa kuzingatia msingi na kanuni maadili katika masuala ya fedha na uchumi.

Maendeleo endelevu ya mwanadamu hayana budi anasema Askofu mkuu Balvo kujikita katika mwelekeo wa kijamii na maisha ya kiroho, kwa wote bila upendeleo, ili kuchangia mustakabali wa mafao na maendeleo ya wengi!









All the contents on this site are copyrighted ©.