2014-07-04 08:51:46

Majadiliano ya kidini yasaidie kupambana na umaskini na ukosefu wa haki msingi!


Ukweli, upendo na huruma ni tunu msingi katika maisha ya waamini wa dini mbali mbali duniani, mambo yanayoweza kumsaidia mwamini kuwa kweli ni chombo cha amani, haki na upatanisho.

Ni changamoto iliyotolewa na Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini alipokutana na kuzungumza na wawakilishi wa dini ya Kihindu, waliokuwa wanaongozwa na Morari Bapu, moja ya wahubiri wakuu wa dini hii, walipomtembelea mjini Vatican.

Waamini wa dini hii wako mjini Roma kushiriki katika warsha inayoongozwa na kauli mbiu “mchakato wa upatikanaji wa amani duniani kwa njia ya mafundisho ya Yesu pamoja na kuangalia mwelekeo chanya kutoka katika Kanisa Katoliki. Warsha hii imeandaliwa na Mfuko wa Lord Dolar Popat kutoka London, Uingereza.

Akichangia katika warsha hii, Kardinali Tauran amekazia umuhimu wa kudumisha tasaufi ya maisha ya kiroho, kwa kuheshimiana; kwa kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu, ili kuimarisha umoja, upendo na mshikamano wa kidugu. Hapa kuna haja kwa waamini wa dini mbali mbali kujenga madaraja kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Majadiliano ya kidini ni nyenzo msingi katika kudumisha umoja, mshikamano na udugu kati ya watu.

Kardinali Tauran anahitimisha kwa kusema kwamba, dini mbali mbali duniani zinaweza kuchangia katika kutafuta na kusimamia mafao ya wengi, kushiriki katika mchakato wa ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika misingi ya haki na amani ya kweli. Hapa kuna haja ya kudumisha utamaduni wa watu kukutana ili kudumisha mshikamano, ili kwa pamoja, waweze kusimama kidete kupambana kufa na kupona na ukosefu wa haki msingi, umaskini na magonjwa.








All the contents on this site are copyrighted ©.