2014-07-04 11:10:54

Kanisa litaendelea kuwasaidia maskini na wagonjwa!


Ugonjwa wa Kifua Kikuu ni kati ya magonjwa yanayoendelea kuhatarisha maisha ya watu wengi duniani, lakini zaidi wale wanaoishi katika Nchi zinazoendelea duniani. Kunako mwaka 1993 Shirika la Afya Duniani lilitangaza mikakati ya kupambana na ugonjwa huu na kuna mafanikio ambayo yameanza kuonekana.

Kati ya mwaka 1995 hadi mwaka 2012, maisha ya watu millioni 22 yaliokolewa na wagonjwa millioni 56 walipata tiba. Haya ni mafanikio makubwa, lakini bado kuna changamoto kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inatokomeza ugonjwa wa Kifua kikuu duniani kwa kutumia dawa makini dhidi ya ugonjwa huu pamoja na magonjwa yanayohusishwa na Ukimwi.


Hayo yamesemwa na Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la wahudumu wa Sekta ya afya wakati alipokuwa anachangia mada kwenye mkutano wa kimataifa kuhusu mikakati ya kutokomeza ugonjwa wa Kifua kikuu katika nchi zile ambazo zina idadi ndogo ya wagonjwa wa kifua kikuu Barani Ulaya. Mkutano huu umefunguliwa mjini Roma, tarehe 4 Julai na unatarajiwa kufungwa rasmi tarehe 5 Julai 2014. Mkutano huu umeandaliwa na Shirika la Afya Duniani kwa kushirikiana na Chama cha Magonjwa ya mfumo wa hewa Barani Ulaya.

Takwimu zinaonesha kwamba, kunako mwaka 2012 kulikuwa na wagonjwa wa Kifua kikuu millioni 8.6, kati yao, wagonjwa millioni 1.3 walifariki dunia. Wengi wao ni watu maskini, wanawake, watoto, wahamiaji, wafungwa watu wasiokuwa na makazi pamoja na wagonjwa wa Ukimwi. Nchi maskini duniani kama vile Afrika na Ulaya ya Mashariki pengine hazifanikiwa kufikia Malengo ya Maendeleo ya Mwaka 2015, kumbe kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuweka mikakati ya kupambana na ugonjwa huu hata baada ya Mwaka 2015.

Mapambano dhidi ya ugonjwa wa Kifua kikuu yawahusishe wadau mbali mbali, ili kuunda kikosi kazi makini kitakachotekeleza mikakati hii kwa ari na kasi kubwa zaidi pamoja na kuyashirikisha Mashirika ya Kidini kwani haya mara nyingi yanafanya kazi katika maeneo ya vijijini na miongoni mwa watu maskini. Kanisa kwa upande wake, litaendelea kuonesha mshikamano na maskini pamoja na wagonjwa kama sehemu ya utekelezaji wa utume wake wa Kinabii na kwamba, hii ni haki jamii. Jamii inayojali haina budu kujenga mahusiano bora na wagonjwa kwa kuwaonjesha huruma kama sehemu ya ubinadamu.

Askofu mkuu Zygmunt Zimowski anawashukuru wadau mbali mbali kwa kushirikisha: ujuzi, maarifa, weledi, muda na rasilimali fedha na watu kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa wanaosumbuliwa na Kifua kikuu sehemu mbali mbali duniani. Bado kuna haja ya kuendeleza mshikamano na huruma kwa wagonjwa wa Kifua kikuu, ili kuendeleza utu na heshima ya binadamu!







All the contents on this site are copyrighted ©.