2014-07-04 11:52:37

"Haki mbinguni, sheria duniani"


Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Mpanda, Tanzania, hivi karibuni ameitaka Familia ya Mungu nchini Tanzania kujivunia kifo cha Sr. Maria Crescentia Kapuli wa Shirika la Bikira Maria Malkia wa Afrika, Jimbo Katoliki Mbeya na wala kisiwakatishe tamaa katika kutekeleza utume wao miongoni mwa Watanzania kwani mauaji haya ya kikatili ni kati ya changamoto ambazo wanapaswa kuzikabili kwa imani na matumaini pasi na kukata tamaa! Amewataka waamini na watanzania kwa ujumla kujenga na kudumisha moyo kusamehe na kuwaombea wauaji ili watubu na kumrudia Mungu.

Aidha Sr.Maria Bilgita Mbanga ambaye ni Makamu Mama mkubwa kutoka Parokia ya makoka na mwalimu wa shule ya mwenyeheri Anwarite ambaye alikuwa na marehemu Sista Cresensia aliyekuwa Mama mkubwa wake hadi mauti yanamkuta ameelezea tukio hilo la kusikitisha.

Akizungumza katika ibada ya misa takatifu ya mazishi katika kanisa la nyumba ya masista Hasamba, Askofu Nyaisonga aliyeongoza misa akiwa na Mhashamu Askofu Evaristus Marcus Chengula (IMC) amesema mateso aliyoyatapa sr.Maria Crescentia yanaashiria alama ya kushinda mauti.

Askofu Nyaisonga ambaye muda wote wa mahubiri yake alionekana kujizuia kulia huku macho yake yakionekana kulengwa na machozi ameiomba Serikali kupitia mamlaka husika kutenda haki katika suala hilo huku akiwasihi wauaji kumrudia Mungu na kutubu ili wawe raia wema. "Masista tukio hili lisiwarudishe nyuma bali liwatie nguvu na kuwa chachu ya utume wenu, muwe kama askari vitani anapopigwa mmoja wengine mnasonga mbele, Sr. Crescentia alifanyakazi katika mazingira yenye changamoto kubwa na alilijuwa hilo, amekufa na Yesu,"alisema.

Alisema waamini wanapaswa kuwasamehe waliotenda uhalifu huo na kuwataka waendelee kuwaombea ili waweze kumrudia Mungu na kuishi kwa amani na kutafuta riziki kwa njia za halali.

Makamu mama mkubwa Sr. Maria Bridgita licha ya kutoa ushuhuda wake katika shamba la Mungu la masista akizungumza na Mwandishi wa habari hizi anasimulia mkasa huo kwa masikitiko makubwa

"Baada ya kusindikizana hadi Benki ya CRDB pale Mlimani City tulikuta wateja wachache Sr. alihudumiwa na baadaye alinipa ishara niende kumsaidia nikafanya hivyo tukahifadhi fedha katika mabegi yetu mawili na nyingine katika bahasha na akampigia simu mkandarasi ambaye aliwasiliana naye tangu tukiwa shuleni kuwa tutamlipia pale pale Benki,"alisema Sr.Bridgita.

Aliongeza,"Tuliona yule Mkandarasi anachelewa kuja Sr.Crescentia akasema twende tukafanye kazi nyingine alafu tukifika shuleni tutampigia aje, lakini tulipokuwa tunatoka karibu na mlango tukakutana naye Mkandarasi tukarudi naye katika chumba maalum tukamkabidhi fedha zake zilizokuwa katika begi langu tukamsainisha tukaaagana naye."

"Tukapanda gari letu kuelekea River Side, Ubungo, Jijini Dar es Salaam ambako tulichukuwa gunia tano za maharage wakati tukiwa katika mafungo Jimboni Mbeya tulimpigia simu mwenye duka hilo apeleke maharage shuleni, baada ya kufika na kuegesha gari pembeni niliteremka na kwenda kulipa Sr. Crescentia na Dreva walibakia ndani ya gari kunisubiri".


"Sikuchelewa sana baada ya kulipa fedha yule mwenye duka alisema ameleta mchele mzuri akanipa kilo mbili za zawadi nikarudi katika gari nikiwa nataka kumuonesha sista mchele ghafla nilisikia mlio kama wa bomu ukitokea upande wangu nikadhani Dereva amegongesha gari nikawa namlaumu naye Dereva alijibu hajagongesha."

"Ghafla walitokea watu watatu na kutuamrisha tusipige kelele na ndipo nilipoingiwa hofu bila kujitambua niliangukia katika mlango wa pili na kujikuta nipo nje ya gari nikijizoa zoa huku mkoba wangu ukiokotwa na mmoja wa wale majambazi nami nikajikuta nimeshikwa na vijana katika duka"

Niliwauliza Sista yupo wapi waliniambia nitulie baadaye wakaja akina mama fulani wakilia na kunitia moyo na nikauliza kimetokea nini na sista yupo wapi wakaniambia amelala amepoteza fahamu lakini baada ya kuwasumbua sana wale vijana wakaniachilia nikaenda lilipo gari nikakuta kundi la watu wamemzingira sista yupo chini amefunikiwa na kitenge huku damu zikitiririka, ilinichanganya zaidi kwani mimi nilijuwa tulikimbia wote mda ule".


Alisema baada ya hapo aliambiwa apige simu kwa wenzake alishindwa ambapo akina mama walimsaidia kuwajulisha kilichotokea na watu wengine waliwapigia Mapadre na baadaye walifika na kunichukuwa huku gari lingine likimbeba sista na wakati nikihojiwa ndipo nilijuwa sista amefariki baada ya Polisi kuulizwa akajibu sista mwenzake marehemu tunaye hapa." Hiyo ndiyo hali halisi ya tukio lilivyotokea na kuchukuwa maisha ya Sista Crescentia, alimaliza kusimulia Sr.Bilgita huku akitokwa na machozi.


Wakizungumza baada ya mazishi baadhi ya waumini wameleezea kifo hicho cha kikatili,kustaajabisha na kuitaka serikali kuchukuwa mkondo wake ili iwe fundisho kwa watu wengine akama ambavyo wazazi kutoka parokia ya Mbalizi na Sr.Anjelina walivyosema kuwa wameshtushwa na mauaji ya kikatili na kinyama aliyofanyiwa Sr.Crescentia mithili ya watu waliokuwa wakilipiza kisasi.

"Labda walikuwa wanamjuwa ndiyo maana wamemuadhibu kiasi hicho lakini kwa nini?, Haingii akilini hata kidogo, maana hata wangempiga kofi tu,"walisema.


Baadhi ya waamini kutoka kanisa kuu la Kiaskofu Parokia ya Mbeya mjini Cotrida Enjewele, Maria Simfukwe, Iporito Mwihava pamoja na Veronica Mwakifuna hawakubaki nyuma kuelezea hisia zao kuhusiana na kifo cha Sista huyo kwa kusema wamebakia njia panda, wamepigwa butwaa na mauaji hayo.

Sisi watanzania wapenda amani na waamini wote wa imani tofauti ambao tunaamini Mwenyezi Mungu yupo, tunadiriki kusema wote waliotenda ama kuhusika katika tukio hilo la kuzima mwanga wa mshumaa wa Sr.Crescentia hapa duniani Mwenyezi Mungu awape nguvu ya kutubu na kumwongokea, lakini pia haki itendeke!

Ninachopenda kusema mauaji ya aina hii hayawezi kuvumilika hata kidogo,sisi watanzania,wapenda amani tunatarajia Jeshi la polisi na vyombo vingine vya dola vitachukuwa hatua madhubuti kuhakikisha watu hao wanapatikana na kufikishwa katika mkono wa sheria.

Sote tunaamini na tunatarajia kusikia kuwa kutokana na umakini na umahiri mkubwa wa maofisa wetu wa vyombo vya dola wahusika watakamatwa, ili mchezo kama huu usije kurudia tena kwa kuwakatili roho watu wa mungu na raia wengine wema.

Nilipoamini kuwa Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya dola vikiamua kweli kufanyakazi na vinafanikiwa ni pale alipouawa aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Liberatus Barow na hata mfano mdogo alipouawa Askari Polisi wa kituo kidogo cha Mkwajuni,wilayani Chunya kwani wahusika na mtandao mzima walikamatwa vivyo hivyo tunavyoamini kwa tukio hili la Mtumishi wa mungu.

Ni rai yangu katika tukio hili Polisi mtende haki katika kuwatafuta na kuwakamata wahusika wa mauaji badala ya kuwakamata vibaka na kuwabambikia kesi kama wanavyoita vijana wa mitaani 'mkawapa kichwa' ili kufunga jarada la upelelezi na hatimaye kutangaza watuhumiwa wamekamatwa.

Mwenyezi Mungu anapenda kuona haki inatendeka licha ya sisi wanadamu tuliopewa dhamana kukengeuka na hata kufikia hatua vijana wa mitaani wakisema haki mbinguni sheria duniani, kwani laana na adhabu tunazionja humu humu duniani za kutotenda haki ila ni siri iliyo katika nafsi na familia zetu.

Wapo baadhi ya askari waliowahi kudhulumu haki za raia wema kwa kuwapatia kesi na matokeo yake maisha yao yamekuwa na laana hivyo tunasihi wahusika wakamatwe na sheria iweze kuchukuwa nafasi yake.

Na Thompson Mpanji, Mbeya, Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.