2014-07-03 12:02:34

Mh. Padre John Bonaventure Kwofie ateuliwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Sekondi-Takoradi, Ghana


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Mheshimiwa Padre John Bonaventure Kwofie wa Shirika la Roho Mtakatifu kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Sekondi-Takoradi, nchini Ghana. Askofu mteule amewahi kuwa Padre mkuu wa Kanda, Shirika la Wamissionari wa Roho Mtakatifu Afrika Magharibi. Alizaliwa tarehe 26 Aprili 1958 huko Powa, Jimbo Katoliki la Sekondi-Takoradi, Ghana.

Baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa, akapadrishwa kunako tarehe 23 Julai 1988, huko Kumasi, Ghana. Katika maisha na utume wake kama Padre, alipangiwa shughuli mbali mbali za kichungaji nchini Gambia na kati ya mwaka 1991 akapelekwa mjini Roma kwa ajili ya masomo ya juu katika Sayansi ya Maandiko Mtakatifu, maarufu kama Biblicum na huko akajipatia shahada ya uzamili.

Amewahi pia kuwa ni Makamu mkuu wa Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume Barani Afrika kwa vipindi viwili; Padre mkuu wa Kanda ya Shirika, Afrika Magharibi, Mratibu wa Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume Barani Afrika, utume alioufanya kazi ya mwaka 2003 hadi mwaka 2005.

Kati ya Mwaka 2004 hadi mwaka 2012 alikuwa ni mshauri wa kwanza wa mkuu wa Shirika la Roho Mtakatifu ulimwenguni. Jimbo la Sekondi-Takoradi lilianzishwa kunako mwaka 1969 na liko chini ya Jimbo kuu la cape Coast, Ghana.







All the contents on this site are copyrighted ©.