2014-07-02 10:37:52

Tanzania yampongeza Papa Francisko kwa kutetea amani duniani!


Askofu mkuu Francisco Montecillo Padila, Balozi wa Vatican nchini Tanzania, Jumatatu tarehe 30 Juni 2014 ameadhimisha Siku kuu ya Watakatifu Petro na Paulo Mitume, kwa kufanya kumbu kumbu ya Mwaka mmoja tangu Baba Mtakatifu Francisko achaguliwe kuliongoza Kanisa Katoliki. Sherehe hii imehudhuriwa na Maaskofu Katoliki Tanzania waliokuwa kwenye mkutano wao mkuu wa mwaka Jijini Dar es Salaam pamoja na viongozi mbali mbali wa Serikali. Sherehe hizi zimefanyika kwenye Ubalozi wa Vatican nchini Tanzania.

Katika hotuba yake, Waziri wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa Bernard Membe amelipongeza Kanisa la Tanzania kwa kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kwa kukazia kwa namna ya pekee kabisa uhuru wa kuabudu! Waziri Membe anasema hakuna amani ya kweli bila ya kuwa na uhuru wa kuabudu.

Serikali ya Tanzania inatambua na kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na Kanisa Katoliki katika ustawi na maendeleo ya watanzania wote katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Kanisa limeendelea pia kuhamasisha umuhimu wa watanzania kusimama kidete kuinda na kutetea amani, kwa kuvumiliana na kuheshimiana katika tofauti zao, wakitambua kwamba, wote ni watoto wa Mungu, tofauti zao ni utajiri mkubwa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watanzania wote.

Waziri Membe anasema anakumbuka kwa namna ya pekee mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro wakati alipokuwa anaanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa kukazia: amani, utunzaji wa mazingira sanjari na kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Anampongeza Baba Mtakatifu kwa kuwahamasisha wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa kutumia ushawishi wao katika kujenga na kudumisha misingi ya amani, upendo na mshikamano wa kimataifa sanjari na kuendeleza majadiliano ili kweli amani na maridhiano kati ya watu yaweze kushika mkondo wake. Baba Mtakatifu ni mtu anayetekeleza kile anachokisema katika uhalisia wa maisha yake kama ilivyojionesha wakati wa hija yake ya kitume katika Nchi Takatifu. Huko aliweza kukutana, kuzungumza na kusali na waamini wa dini mbali mbali na hatimaye, hivi karibuni aliweza kuwaalika Marais wa Israeli na Palestina mjini Vatican kwa ajili ya kuombea amani huko Mashariki ya kati.







All the contents on this site are copyrighted ©.