2014-07-02 08:45:33

Kanisa litaendelea kusimamia maadili na utu wema!


Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa nchini Tanzania, hivi karibuni yaliadhimisha Kongamano la Nne la Utoto Mtakatifu, lililofanyika Jimboni Tunduru Masasi. Tukio hili liliwakusanya watoto wa Utoto Mtakatifu, walezi pamoja na Maaskofu kutoka Majimbo mbali mbali nchini Tanzania. RealAudioMP3

Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania aliwataka watoto kusali na kuendelea kuwa ni mabalozi na wajenzi wa misingi ya haki na amani. Sala za watoto wadogo zinasikilizwa sana na Mwenyezi Mungu, kumbe ni wajibu wao kusali ili Mwenyezi Mungu aweze kuwajalia walimwengu haki na amani, kwani kwa sasa watu wengi wanalilia na kutamani amani ya kweli, ingawa pia kuna watu wanaoichezea amani kwa kuendekeza mambo yasiyokuwa na mashiko wa tija kwa maendeleo na ustawi wa wananchi wengi.

Askofu mkuu Damian Dallu wa Jimbo kuu la Songea ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Uinjilishaji Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, aliwataka watoto wa Utoto Mtakatifu kuhakikisha kwamba, wanatumia vyema akili, ujuzi na maarifa yao kuhusu Mungu kwa ajili ya maisha yao kwa sasa na ustawi wa Kanisa na Tanzania kwa siku za usoni. Watoto wanawajibika kutumia vyema muda na fursa zao mbali mbali kwa ajili ya maendeleo yao binafsi, Kanisa na Jamii inayowazunguka na wala si vinginevyo.

Ni matumaini ya washiriki wa kongamano hili kwamba, baada ya maadhimisho haya, Jamii itakuwa na mtazamo na mang’amuzi bora zaidi katika mchakato wa maboresho ya maisha ya watoto. Watoto ni matumaini ya Kanisa na taifa kwa leo na kesho, hivyo wanapaswa kuheshimiwa, kulindwa, kuthaminia na kupewa mahitaji yao msingi yanayojikita katika: elimu bora, afya, chakula, malazi, mavazi na malezi makini. Watoto ni matumaini na jeuri ya Kanisa, ndiyo maana Kanisa linaendelea kuwekeza kwa dhati kabisa katika maisha na utume wa watoto ili nao waweze pia kuwa ni wadau wa Uinjilishaji miongoni mwa watoto wenzao.

Kwa upande wake, Askofu Renatus Nkwande wa Jimbo Katoliki Bunda anasema, Kanisa litaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea ukweli, utu wema na maadili ndani ya Jamii. Askofu Nkwande ameyasema hayo wakati alipokuwa anazungumza na walezi wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa nchini Tanzania. Anasema, Kanisa litaendelea kukazia umuhimu wa Jamii kudumisha misingi ya maadili na utu wema; litakemea mmong’onyoko wa maadili kwa macho makavu kabisa bila kusita wala kuogopa, kwa mambo yale yanayokwenda kinyume cha mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Askofu Nkwande anasema, Kanisa litaendelea kupinga ndoa za watu wa jinsia moja, kwani mwelekeo huu ni kinyume kabisa cha utu na heshima ya binadamu; unakwenda kinyume na mila na tamaduni za Kiafrika na kwamba, ni kinyume kabisa cha mpango wa Mungu kwa mwanadamu. Kanisa Katoliki litaendelea kuwahimiza waamini na watu wote wenye mapenzi mema kulinda, kutetea na kutangaza Injili ya Uhai dhidi ya utamaduni wa kifo unaokumbatiwa na sera za utoaji mimba na kifo laini au Eutanasia. Hii inatokana na ukweli kwamba, maisha ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na mwanadamu amekabidhiwa kulinda, kuitunza na kuiendeleza.

Kanisa linawahimiza wazazi na walezi kutekeleza dhamana na wajibu wao katika malezi na makuzi ya watoto kadiri ya mafundisho ya Kanisa, mila na desturi njema za Kiafrika. Wazazi wawajibike barabara katika malezi ya watoto wao na kamwe wasiachie mitandao ya kijamii kuwa ni walezi mbadala baada ya wazazi kushindwa kutekeleza wajibu wao kikamilifu.

Askofu msaidizi Titus Mdoe wa Jimbo kuu la Dar es Salaam alipokuwa anatoa nasaha kwa wazazi na walezi wa Utoto Mtakatifu kama sehemu ya maandalizi ya Kongamano la Utoto Mtakatifu lililofanyika Jimbo Katoliki la Tunduru Masasi alisema kwamba, hatima ya Kanisa na taifa iko mikononi mwa familia zenyewe. Hii inategemea jinsi familia zinavyojihusisha kwa malezi na makuzi ya watoto wao; kwa kuwajengea watoto hawa msingi wa tunu bora za maisha na uchaji wa Mungu, wakitambua kwamba, wanapanda mbegu ya maisha ya kimissionari kwa watoto hawa kwa siku za usoni.

Watoto waliofundwa na kufundika, ni msingi bora wa Jamii inayowajibika na kusimamia mafao ya wengi. Watoto wapewe malezi bora, waheshimiwe na kuthaminiwa na kamwe, wasidhulumiwe wala kunyanyaswa na watu waliokengeuka na kupotoka kimaadili. Wazazi wawaonjeshe watoto wao fadhila ya imani, matumaini na mapendo; watoto wao ni mwelekeo chanya wa maisha na kamwe wasiwe ni watu waliokata tamaa kwani matokeo yake ni kutumiwa na baadhi ya watu katika jamii kusababisha kinzani na uvunjifu wa amani, kama inavyojitokeza sehemu mbali mbali za dunia.

Naye Padre Timoth Maganga, Mkurugenzi wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa Jimbo kuu la Dar es Salaam, anawataka wazazi kuhakikisha kwamba, wanawarithisha watoto wao imani na kweli za Kiinjili kadiri ya mafundisho ya Kanisa Katoliki. Licha ya kuhakikisha kwamba, watoto wanapata elimu bora, afya njema, malazi na makazi bora, wawajengee pia msingi bora wa maisha ya kiroho kwa kuwashirikisha fadhila ya imani, matumaini na mapendo, ili kweli mwisho wa siku, watoto hawa waweze kuwa ni Wachamungu na raia wema; watu wanaotegemewa na Jamii.

Wazazi waoneshe mifano bora kwa njia ya ushuhuda wa imani katika matendo. Wajitahidi kupandikiza mbegu ya miito mbali mbali katika maisha ya watoto wao. Watoto wanaoonesha nia ya kuwa Mapadre na Watawa wasaidiwe na wazazi pamoja na walezi wao kutambua sauti ya Mungu katika maisha ya watoto hawa kwa siku za usoni. Wazazi wajitahidi kukaa na kuishi na watoto wao, ili watoto hawa mwisho wa siku waweze kupata ukomavu wenye uwiano bora katika maisha yao. Watoto wapate malezi bora kutoka kwa Baba na Mama; Walimu na kutoka katika Kanisa kwa ujumla.

Kongamano la Kitaifa la Utoto Mtakatifu hufanyika kila baada ya miaka miwili. Kwa mara ya kwanza Kongamano hili lilifanyika Jimboni Iringa, likafuatia Jimbo Katoliki la Zanzibar na Mwaka 2011 Jimbo Katoliki Ifakara likawa Mwenyeji wake.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.