2014-07-02 16:38:56

Baraza la Makardinali linaendelea na kazi yake!


Baba Mtakatifu Francisko pamoja na Baraza la Makardinali, Jumatano wameendelea na kikao chao kadiri ya ratiba kwa kuangalia shughuli na utendaji wa mji wa Vatican kama taarifa ilivyowasilishwa na Bertello na kuhusu Sekretarieti ya Vatican kama ilivyowasilishwa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican. Baraza la Makardinali limepembua tena hali na mwenendo wa Benki ya Vatican kwa kuwashirikisha Makardinali wanaosimamia Benki hii ambao kwa sasa wako mjini Roma.

Akizungumzia kuhusu habari zinazoendelea kusikika kwenye vyombo vya habari kuhusu Benki ya Vatican, IOR, Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Benki ya Vatican iko katika kipindi cha mpito na mageuzi yanayofanyika kwa hali ya utulivu. Mchango unaotolewa na Bwana Ernst Von Freyberg ni muhimu na umepokelewa kwa mikono miwili. Bado kutakuwa na maelezo zaidi baada ya kukamilika kwa Baraza la Kipapa la Uchumi, linalotarajia kufanya mkutano wake, Jumamosi ijayo, baada ya mkutano huo, maendeleo zaidi yataweza kuwekwa hadharani.

Baraza la Kipapa la Uchumi utawasilisha bajeti ya Vatican kwa mwaka 2013 - 2014. Juma lijalo, kutakuwepo na mkutano mkubwa wa waandishi wa habari ili kuelezea kwa kina na mapana yale yatakayojiri katika mkutano wa Baraza la Makardinali unaoendelea kwa sasa mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.