2014-07-01 08:40:42

Wanawake simameni imara kupambana na nyanyaso za kijinsia!


Wachunguzi wa masuala ya nyanyaso dhidi ya wanawake katika maeneo ambamo mtutu wa bunduki unaoekana kutawala zaidi wanabainisha kwamba, dini kwao ni sawa na upanga wenye makali kuwili, katika baadhi ya maeneo ambamo dini inachukuliwa kama sehemu ya siasa, viongozi wa kidini na taasisi zao hawakuwa na mchango madhubuti katika kuwasaidia wanawake waliokumbwa na nyanyaso pamoja na dhuluma wakati wa vita na machafuko ya kijamii. RealAudioMP3

Lakini utafiti unaonesha kwamba, pale ambapo dini zimekuwa mstari wa mbele kuwasaidia waamini wao katika mahangaiko wakati wa vita na machafuko ya kidini, zimekuwa msaada mkubwa katika kuimarisha imani, matumaini na mapendo miongoni mwa wanawake, kiasi kwamba, wameendelea kuwa kweli ni mashahidi wa imani tendaji. Kwa njia ya imani, wanawake hawa wameweza kujikita katika mchakato wa kuponya madonda ya nyanyaso na dhuluma yaliyokuwa yamejificha katika maisha yao!

Haya yamebainishwa hivi karibuni katika semina iliyoandaliwa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni na kuratibiwa na Dr. Fulata Lusungu Moyo. Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa katika maamuzi yake, linaendelea kuwahamasisha wanawake kushiriki kikamilifu katika mchakato wa ujenzi wa misingi ya haki na amani katika maeneo ambamo vita na machafuko ya kijamii yameshamiri kwa muda mrefu. Kwa njia hii wanaweza kusaidia ujenzi wa haki jamii kwa kuzingatia usawa wa kijinsia. Katika vita na machafuko ya kijamii, wanawake na watoto ndio wanaoathirika zaidi.

Majukwaa ya kijamii na vyama vya kiraia ni fursa nzuri kwa wanawake kuweza kujipanga vyema kukabiliana na mustkabali wa maisha yao kwa pamoja, kwani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Mafanikio haya yamejionesha kwa namna ya pekee kwa vyama vya wanawake Afrika Mashariki katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita. Mahali ambapo wanawake wanashirikishwa kikamilifu katika kupanga na kuamua hatima ya maisha ya kijamii, wamekuwa mstari wa mbele katika kupigania na kutetea haki msingi za wanawake katika Jamii.

Ni wanawake wanaotaka kuona kwamba, jamii inajengeka katika misingi ya usawa, haki na kuheshimiana, ndiyo maana kuna umuhimu pia wa kujenga na kudumisha majukwaa ya majadiliano ya kidini na kiekumene miongoni mwa wanawake, ili kwa pamoja licha ya tofauti zao za kiimani, waweze kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya wanawake wote, tayari kujifunga kibwebwe kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watu wao.

Uponyaji wa madonda ya nyanyaso na dhuluma wanazofanyiwa wanawake katika maeneo ya vita na machafuko ya kijamii ni mchakato unaojikita katika hija ya maisha ya mtu binafsi kiroho pamoja na kushirikishana na wengine katika vyama na majukwaa ya kijamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.