2014-07-01 09:12:39

Papa kutembelea Jimbo la Molise, tarehe 5 Julai 2014


Baba Mtakatifu Francisko Jumamosi tarehe 5 Julai 2014 anatarajiwa kutembelea Jimbo Katoliki la Molise, lililoko Kusini mwa Italia. Hii itakuwa ni mara yake ya tano kutembelea Majimbo Katoliki nchini Italia. Atakapowasili Jimboni humo atazungumza na wafanyakazi kutoka katika Mkoa wa Molise, baadaye saa 4:30 asubuhi ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na baadaye atakwenda kwenye Kanisa kuu ili kusalimiana na wawakilishi wa wagonjwa kutoka Molise.

Kama kawaida, Baba Mtakatifu atapata chakula cha mchana na maskini wanaohudumiwa na Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki Campobasso na baadaye atakutana na vijana wa kizazi kipya kutoka Abruzzo na Molise. Baba Mtakatifu, baadaye ataelekea mjini Isernia anakotarajiwa kukutana na kuzungumza na wafungwa wanaotumikia adhabu zao mbali mbali gerezani humo. Akiwa mjini humo atakutana na kusalimiana na wagonjwa. Jioni, Baba Mtakatifu anatarajiwa kukutana na wananchi wa Isernia na hapa atatangaza Mwaka wa Jubilee ya Celestini.

Baada ya shughuli zote hizi, Baba Mtakatifu anatarajiwa kurejea tena Vatican kuendelea na kipindi chake cha mapumziko na kazi! Kama kawa, Idhaa ya Radio Vatican itakuwa nawe bega kwa bega kukuza yale yanayojiri katika matukio kama haya!







All the contents on this site are copyrighted ©.