2014-06-30 15:15:01

Kanisa litaendelea kusimamia mafao ya wengi!


Askofu mkuu Franco Coppolla aliyeteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Balozi Mpya wa Vatican nchini Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, hivi karibuni aliwasili nchini humo na kupokelewa na viongozi wa Kanisa Afrika ya Kati. RealAudioMP3

Baadaye, Askofu mkuu alipeleka nakala za hati zake za utambulisho kwa Waziri wa Mawasiliano na Upatanisho wa Kitaifa toka Jamhuri ya Afrika ya Kati Bwana Antoinette Montaigne anayekumbuka kwamba, tarehe 29 Juni 2013 alishiriki katika Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican wakati alipokuwa anatoa Palio Takatifu kwa Maaskofu wakuu, mmoja wapo akiwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Bangui.

Baadaye Askofu mkuu Coppola aliwasilisha pia hati zake za utambulisho kwa Rais Catherine Samba-Panza, Rais wa Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati aliyekuwa ameambatana na viongozi wakuu waandamizi nchini humo.

Rais Samba-Panza amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kujali mateso na mahangaiko ya wananchi wa Afrika ya Kati, ambao wamepitia kipindi kigumu cha vita ya wenyewe kwa wenyewe pamoja na misigano ya kijamii iliyosababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao. Anashukuru pia mchango mkubwa uliofanywa na Kanisa Katoliki katika kuwahudumia wananchi waliokuwa wamepoteza matumaini kutokana na vita.

Kwa upande wake, Askofu mkuu Franco Coppola anasema, Kanisa Katoliki, litaendelea kushikamana kwa dhati na wananchi wote wa Jamhuri ya Afrika ya Kati ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na mshikamano wa kitaifa, kwa ajili ya mafao ya wengi.

Askofu mkuu Coppola, aliwasilisha nakala za hati zake za utambulisho kutoka kwa Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwa Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati.








All the contents on this site are copyrighted ©.