2014-06-30 12:31:12

Jubilee ni kipindi cha shukrani na toba!


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na Askofu wa Jimbo Katoliki la Iringa, tarehe 1 Julai 2014 anasherehekea kilele cha Jubilee ya miaka 25 ya Uaskofu. Itakumbukwa kwamba, Askofu Ngalalekumtwa alizaliwa tarehe 25 Oktoba 1948 huko Iringa. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapadrishwa tarehe 17 Aprili 1973.

Tarehe 14 Novemba 1988 akateuliwa na Mtakatifu Yohane Paulo II kuwa Askofu mwandamizi wa Jimbo Katoliki Sumbawanga. Tarehe 6 Januari 1989 akawekwa wakfu kuwa Askofu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican na Papa Yohane Paulo II. Tarehe 21 Novemba 1992 akateuliwa kuwa ni Askofu wa Jimbo Katoliki Iringa.

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu Ngalalekumtwa anasema, Mwenyezi Mungu amempatia fursa katika kipindi cha miaka 25 kuwafundisha, kuwatakasa na kuwaongoza watu wa Mungu katika njia za haki na uadilifu katika Bwana. Amejitahidi kutumia muda, nguvu na vipaji vyake kwa ajili ya ustawi wa Kanisa na maendeleo ya binadamu.

Anasema furaha kubwa kwa mchungaji ni pale anapojituma bila ya kujibakiza kwa ajili ya watu wake; ni ile hali ya kushiriki katika furaha na machungu ya watu wake kwa kutambua kwamba, hata yeye ni sehemu ya Familia ya Mungu. Katika maisha amekabiliana na changamoto nyingi kama vile uchovu, magumu ya maisha, vipindi vya majaribu kwa mtu binafsi, kwa Kanisa na Jamii husika. Katika hali kama hii kunahitajika utulivu, sala na maombi kutoka kwa watu mbali mbali.

Jubilee ya miaka 25 ya Uaskofu ni kipindi cha kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai na yote aliyomwezesha kutekeleza katika kipindi chote hiki. Jubilee ni kipindi cha kuomb toba na msamaha kwa mapungufu ya kibinadamu, kwani Mwenyezi Mungu ni mwingi wa huruma, mapendo na msamehevu. Anamwomba Mungu amzidishie neema na baraka pale alipofanya vyema, amhurumie pale alipomsaliti.







All the contents on this site are copyrighted ©.