2014-06-29 14:37:25

Vita inazaa vita, majadiliano ni njia ya amani!


Mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 29 Juni 2014, Baba Mtakatifu Francisko aliyaelekeza mawazo yake huko Iraq ambako habari za kusikitisha na kutia uchungu na simanzi zinaendelea kusikika kila kukicha!

Baba Mtakatifu anasema, anapenda kuungana na Maaskofu mahalia kuwataka viongozi wa Serikali kuanzisha mchakato wa majadiliano, ili umoja na mshikamano wa kitaifa uweze kutawala na hatimaye, kushinda kishawishi cha kutaka kujitumbukiza katika vita ya wenyewe kwa wenyewe.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, yuko karibu na familia zote zinazoteseka nchini Iraq, lakini kwa namna ya pekee kabisa yuko karibu na Familia za Kikristo ambazo zinalazimika kuyahama makazi yao kutokana na hatari inayowazunguka. Vita inazaa vita nyingine, majadiliano ni njia pekee ya ujenzi wa misingi ya amani.

Baba Mtakatifu amewakumbuka na kuwasalimia ndugu, jamaa, marafiki na waamini waliohudhuria kwenye Ibada ya Misa Takatifu ili kuwasindikiza Maaskofu wakuu 27 waliovishwa Pallio Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Anawapongeza wasanii waliopamba mji wa Roma kwa maua kama sehemu ya maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu Petro na Paulo, wasimamizi wa Roma.

Anawashukuru waamini wote wanaoshiriki kwa ukarimu kuchangia Mfuko wa Ukarimu wa Papa kwa ajili ya kuwasaidia watu wanaokumbwa na majanga mbali mbali katika maisha. Anawatakia kheri na baraka wanaojibidisha kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa kituo cha michezo katika Nchi Takatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.