2014-06-27 11:08:30

Wanafunzi jengeni nyumba ya amani na upendo!


Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki, Alhamisi jioni tarehe 26 Juni 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kama sehemu ya kumbu kumbu ya miaka 40 tangu kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Bethlehemu. Ibada hii imewashirikisha wajumbe wa bodi ya wadhamani na baadhi ya wanafunzi, ambao pia walipata bahati ya kuhudhuria Katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko, siku ya Jumatano.

Kardinali Sandri katika mahubiri yake amekazia kuhusu umuhimu wa Fumbo la Msalaba, linaloonesha jinsi ambavyo Yesu mwenyewe alijisadaka na kuwakirimia wanafunzi wake chakula cha uzima wa milele na Roho Mtakatifu, anayewawezesha kuwamegea wengine upendo kama unavyojionesha katika Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Bethelehemu.

Huu ni ushuhuda wa imani tendaji, unaojionesha kwa majitoleo ya watu mbali mbali ili kuhakikisha kwamba, vijana wanapata elimu itakayowawezesha kuwa na utimilifu wa maisha. Hii ni changamoto na mwaliko wa kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu na kwa binadamu, kwa kuendeleza juhudi za kuwapatia vijana elimu, kwa utukufu wa Mungu unajionesha kwa mwanadamu aliye hai.

Kardinali Sandri anasema kwa njia ya upendo kwa Kristo na vijana wa dini mbali mbali wanaosoma Chuo hapo, Kanisa linatekeleza dhamana ya kuwajengea vijana matumaini na kwamba, vijana nao wahakikishe kuwa hakuna mtu anayewapora matumaini haya kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko. Chuo kikuu kiwe ni mahali pa ujenzi wa misingi ya haki, amani, umoja na upatanisho wa kitaifa. Vijana wanaofundwa chuoni hapo wahakikishe kwamba, wanabomoa kuta za utengano kati ya watu na badala yake upendo na amani vitawale mioyo ya watu!







All the contents on this site are copyrighted ©.